Wauguzi wakimbia nyumba za zahanati


Claudia Kayombo, Kibaha

IMANI za kishirikina zimetajwa kuwa chanzo cha kukimbiza waganga na wauguzi wa zahanati ya Viziwaziwa, kwenye nyumba zilizojengwa eneo hilo kwa ajili yao.

Zahanati hiyo iliyoko wilayani hapa, wafanyakazi wake wanadaiwa kukimbia nyumba mbili, badala yake sasa wanaishi Dar es Salaam na hapa.

Hayo yalibainika hivi karibuni baada ya JAMBO LEO kuzuru eneo hilo na kubaini changamoto hiyo kwa wananchi wa mitaa minne ya kata ya Viziwaziwa wanaotegemea zahanati hiyo.

Diwani wa Kata hiyo, Mohamed Chamba na Ofisa Mtendaji wa Kata ya Viziwaziwa, Said Mtindo walithibitisha madai hayo na kubainisha kuwa hakuna ukweli wowote bali ni dhana tu.

Chamba alisema ni kweli hakuna mganga wala muuguzi anayeishi kwenye nyumba hizo za zahanati na kwamba, hatua hiyo inawapa shida wananchi wanaopangiwa sindano za saa au wanaougua ghafla usiku.

“Baada ya saa 9:30 alasiri hapa hakuna mganga wala muuguzi, mtu akishikwa na homa ya ghafla anatakiwa kwenda Kwa Mathias, hulazimika kusafiri kwa bodaboda kwa gharama ya kati ya Sh 5,000 na Sh 10,000 ambazo ni mzigo mkubwa, hofu yangu wakati huu tunapoelekea masika, wananchi watapata shida sana,” alisema Chamba.

Ofisa Mtendaji huyo alifafanua kuhusu madai hayo ya ushirikina akisema hakuna ukweli wowote.

Akifafanua, alisema kuliwahi kuwa na madai kwamba aliyewahi kuwa muuguzi kwenye zahanati hiyo alipotelewa na mjukuu wake katika mazingira ya utata, lakini baadaye ikajulikana kuwa alitorokea kwa ndugu zake.

Alisema viongozi wa wilaya hiyo akiwamo Mbunge wa Viti Maalumu walikutana na wafanyakazi hao wa afya na kuwashawishi waondokane na dhana hiyo, lakini hawajaonesha nia ya kurudi.

Alisema jitihada za Serikali kushawishi wafanyakazi hao wa afya zinaendelea na sasa inaunganisha huduma ya maji ili kumaliza changamoto ambazo zinaweza kuwa sababu ya wao kutohamia kwenye nyumba hizo.

Mganga wa Zahanati hiyo, Adriene Oringo, alipoulizwa kuhusu madai hayo, alisema hawezi kuzungumza lolote kwa kuwa suala hilo liko ngazi za juu.

Kaimu Mkurugenzi wa Halmashauri ya Kibaha, Amkauane Ngilangwa, alisema hajui chochote kuhusu jambo hilo kwa kuwa amekaimu nafasi hiyo kwa muda mfupi tu.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo