Mabasi ya mikoani yaadimika Ubungo


Hussein Ndubikile

ZIKIWA zimebaki siku tatu kusherehekea Sikukuu ya Krismasi, abiria wa mabasi yaendayo mikoani wamekwama kwenye kituo cha mabasi ya mikoani cha Ubungo, Dar es Salaam na kulazimika kutumia usafiri wa daladala aina ya Eicher kwenda mikoa ya Kaskazini na Kanda ya Ziwa.

Uchunguzi uliofanywa na gazeti hili kwenye kituo hicho ulibaini kuwapo kwa daladala hizo zilizokuwa na abiria wakielelea mikoa ya Arusha, Kilimanjaro, Mwanza na Kagera.

Dereva wa moja ya mabasi hayo, Rashid Msangi alisema huduma ya usafiri wa mabasi kituoni hapo imeadimika kutokana na abiria   kuongezeka kuanzia juzi (Jumanne) na jana, hali iliyosababisha kuomba vibali na kukaguliwa na wakaguzi wa kikosi cha polisi wa usalama barabarani.

"Abiria wameongezeka, juzi walianza kuondoka na daladala hizi leo (jana) ndio kama unavyowaona hawa, wanaelekea Arusha na Moshi," alisema.

Alisema kwa safari za mikoa hiyo huwatoza nauli ya kati ya Sh 25,000 na Sh 28,000 kufuatana walivyoelekezwa na Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Nchi Kavu na Majini (Sumatra) na Chama cha Kutetea Abiria nchini (Chakua).

Wakala wa kampuni ya Happy Nation, Swalehe Yasin alisema tatizo hilo limetokea kwa watu wa mikoa hiyo kutosafiri mapema kama ilivyozoeleka, huku akiongeza kuwa ugumu wa maisha nao umechangia hali hiyo.

Yasin alisema tiketi za mabasi yanayokwenda mikoa hiyo zimekwisha, hivyo kwa abiria anayehitaji anatakiwa kwenda kituo hicho cha mabasi Jumapili.

Abiria Hassan Issa aliyekuwa akielekea Arusha alisema alifika kituoni hapo saa 2 asubuhi na kukuta mabasi yamejaa hali iliyomlazimu kusubiri usafiri wa daladala hizo.

Abiria wa Korogwe, Tanga, Mwanakhamisi Ramadhan alisema alipata adha kubwa ya usafiri kutokana na mabasi kuwa machache na aliyoyakuta kujaa abiria.

Ofisa Elimu wa Chakua, Gervas Rutaguzinda alisema uhaba wa mabasi umetokana na idadi ya abiria kuongezeka na kulazimika kutafuta njia mbadala ya kusaidia abiria wanaokwenda mikoa hiyo kwa kuleta daladala zinazofanya safari za Gongo la Mboto, Tegeta, Mbagala na Kibaha.

Kwa mujibu wa Kamanda wa Kikosi cha Usalama Barabarani nchini, Mohamed Mpinga kikosi chake imejipanga kudhibiti ajali za barabarani kwa kuongeza askari na utozaji wa nauli wa kiholela.

Kamanda Mpinga alisema daladala zinazobeba abiria Ubungo hazifanyi safari bila kukaguliwa na wakaguzi wa kikosi hicho.  
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo