CCM yaanza kuhakiki mali za chama


Sharifa Marira

Makao Makuu ya CCM Dodoma
CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) Mkoa wa Dar es Salaam kimeanza uhakiki wa mali zake ambapo hadi sasa kimehakiki kata 40 huku kikitarajia kupitia kata 102.

Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Katibu wa Itikadi na Uenezi wa Mkoa, Juma Gadafi alisema lengo la uhakiki huo ni kutekeleza maagizo ya chama na kuboresha utendaji.

‘’Tunaendelea na uhakiki wa mali za chama, tumeshapita kata 40 lengo ni kata zote 102 ambazo tuna imani hivi karibuni tutakamilisha uhakiki ili kuboresha utendaji wa chama,’’ alisema Gadafi.

Katika hatua nyingine, chama kimempitisha Tausi Milanzi kuwa mgombea udiwani kata ya Kijichi na kwamba kinatarajia kupata ushindi wa kishindo kutokana na sera za CCM kutetea wanyonge na mgombea wake anatarajiwa kuchukua fomu kesho.

Alisema Serikali ya CCM imefanya kazi kubwa ya utekelezaji wa Ilani ya chama, hivyo hapana shaka wananchi kuunga mkono ushindi wa chama hicho kata ya Kijichi, ili kuendeleza utekelezaji wa ahadi zake.

“Kamati ya Siasa ya Mkoa ilipokea majina 12 ya wagombea udiwani wa kata ya Kijichi waliotokana na kura za maoni kwa kuzingatia kanuni na sheria, tumemteua Milanzi kupeperusha bendera na tuna imani atakwenda kusimamia utekelezaji wa Ilani,’’ alisema Gadafi.

Akizungumzia uteuzi wa nafasi ndani ya CCM uliofanywa hivi karibuni na Mwenyekiti wake, Rais John Magufuli alisema umezingatia mahitaji ya chama hicho, katika kupigania maslahi ya wananchi.

Alisema kutokana na safu ya uongozi iliyopo inawataka wahujumu maendeleo kwa makusudi ikiwemo wanaokwepa kulipa kodi na kuacha mara moja kwa kuwa hawatakuwa na pa kukimbilia.

“CCM iliyopo ni ya kisayansi na imefanya mkutano wake wa Kamati Kuu na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) kwa siku moja lakini kulitoka na uamuzi mzito wenye maslahi makubwa kwa chama na kwa sasa tunasubiri Mkutano Mkuu upitishe maazimio hayo na kuanza utekelezaji wake,” alisema.

Alisema CCM Mkoa itahakikisha inashirikiana na kufanya kazi na viongozi walioteuliwa ili kuleta ufanisi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo