Sheria ya Ndoa inachangia mimba za utotoni


Grace Gurisha

TAASISI ya Utawala Bora na MaendeleoTanzania (Cegodeta), imeiomba Serikali kubadilisha Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971 haraka au kuifuta kabisa kwa sababu inakinzana na Sheria ya Mtoto.

Mkurugenzi mtendaji wa taasisi hiyo, Thomas Ngawaiya alieleza kuwa sheria hiyo ilitakiwa ifutwe kutokana na kwamba inagongana na Sheria ya Kimataifa ya Mwaka 2004 ambayo Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania liliridhia kuwa mtu wa chini ya umri wa miaka 18 ni mtoto.

“Baada ya kupitisha sheria hiyo Bunge lilitakiwa irekebishe Sheria ya Ndoa ya Mwaka 1971, lakini halikufanya hivyo jambo ambalo linaipa Mahakama wakati mgumu kwenye kuamua kesi za watoto wa chini ya miaka 18 kuolewa.

“Mahakama inaweza kuamua chochote kwa kuwa sheria inaruhusu mtoto huyo kuolewa na hivyo kuchangia mimba za utotoni. Lakini hiyo ni kinyume na haki za mtoto wa kike kwa sababu na yeye ana haki ya kusoma kama mtoto wa kiume,” alisema Ngawaiya.

Alisema wanaishauri Serikali kuchukua hatua za makusudi zinazolenga kufanikisha utoaji wa elimu kwa watoto wa kike wanaopata ujauzito na kujifungua kabla ya kuhitimu masomo yao.

Pia, alisema wamefikia hatua hiyo kufuatia utafiti iliyoufanya na kubaini changamoto mbalimbali zinazohitaji kutatuliwa kwa haraka ili kujenga taifa lenye nidhamu kwa ngazi zote. Alisema hatua hiyo itawawezesha wale waliokumbwa na mikasa ya ujauzito kurejea mashuleni, ambapo pia itakuwa ni fursa nyingine ya kupata elimu ya malezi ya watoto wao.

“Ili mtoto huyu aliyejifungua arudi shuleni kuendelea na masomo ni vyema kuwe na madarasa maalumu kwa ajili hiyo tu au zijengwe shule moja moja kwa kila wilaya, zikiwalenga watoto hawa ili waweze kupata masomo ya ziada ya malezi ya mtoto”, alisema.

Ngawaiya alisema idadi ya watoto wanaopata ujauzito shuleni haizidi asilimia 10, hivyo ametaka kuwepo hatua za makusudi ili kupunguza idadi hiyo, sanjari na kuendelea kutoa adhabu kali kwa wale wanaobainika kuwapa mimba wanafunzi bila kujali nyadhifa zao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo