Bosi Jamii Forums arudishwa rumande


Grace Gurisha

Maxence Melo
MMILIKI wa mtandao wa Jamii Forums, Maxence Melo, amepandishwa kizimbani mara tatu kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam akikabiliwa na mashitaka manne likiwamo la kuzuia upelelezi wa Polisi kuhusu mtandao huo.

Ilikuwa kama sinema jana, kwani Melo alipandishwa kwa mahakimu watatu tofauti na kila alipopata dhamana kwa hakimu mmoja, askari walimkamata na kumrudisha mahakamani kwa hakimu mwingine na kusomewa mashitaka mengine, kabla ya kushindwa masharti kwa hakimu wa tatu.

Baada ya Melo kutoka kwa hakimu huyo na kurudishwa mahabusu mahakamani hapo, alichukuliwa na gari la Polisi na kuondolewa eneo hilo, akiwa chini ya ulinzi wa askari zaidi ya sita.

Melo alionekana mwenye huzuni akiwa amekalishwa chini kwenye gari hilo.

Hatua hiyo ilifikiwa na Jeshi hilo baada ya Melo kushindwa kutimiza masharti ya dhamana katika kesi ya mwisho kati ya tatu alizoshitakiwa kwa wakati mmoja, ambapo alitakiwa awe na wadhamini wawili wa kuaminika waliotakiwa kusaini bondi ya Sh milioni tano kwa kila mmoja.

Mashitaka

Melo ambaye ni Mkurugenzi wa Jamii Media Co Ltd, alipandishwa kizimbani kwa mahakimu wakazi watatu, Mwandamizi Thomas Simba, Victoria Nongwa na Godfrey Mwapamba.

Wakili wa Serikali, Mohamed Salum alidai mbele ya Simba kuwa katika tarehe zisizofahamika kati ya Aprili mosi na Desemba 13, akiwa Mikocheni, Dar es Salaam akiwa Mkurugenzi wa Jamii Media na mwendeshaji wa Jamii Forums, alizuia upelelezi.

Alidai kuwa akiwa katika ofisi hizo akifahamu kuwa Polisi inafanya uchunguzi wa makosa ya mtandao kupitia tovuti yake kuona kama alikiuka Sheria ya Mitandao, alikataa kutoa taarifa za elektroniki.

Melo akiwa mbele ya Hakimu Mwambapa, alidaiwa kuwa tarehe zisizofahamika kati Mei 10 na Desemba 13, akiwa eneo hilo, alizuia upelelezi wa Polisi kwa kukataa kutii amri za kutoa taarifa za mtandao wake.

Katika kesi ya tatu, Melo alipandishwa kizimbani kujibu tuhuma mbili mbele ya Hakimu Nongwa; kuzuia uplelezi na kuendesha mtandao  bila kuusajili.

Salum alidai kuwa siku zisizofahamika kati ya Desemba 9, 2011 na Desemba 13 mwaka huu, akiwa Mikocheni, aliendesha mtandao wa ‘jamiiforums.com’ bila kusajiliwa na mtandao wa Tanzania (do-tz).

Dhamana

Baada ya Melo kusomewa mashitaka alikana kuhusika, na upande wa Jamhuri kudai kuwa upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika na kuomba siku nyingine ya kutajwa kesi hizo, huku ukidai kuwa hauna pingamizi la dhamana kwa mshitakiwa.

Mawakili wa Melo, Jebra Kambole na Mtobesya, waliiomba Mahakama impe dhamana mteja wao kwa sababu tuhuma zake kisheria zinadhaminika na pia ni haki yake kupata dhamana, hivyo kuomba masharti nafuu.

Hakimu Simba alisema ili awe nje kwa dhamana, alitakiwa awe na wadhamini wawili wa kuaminika, kila mmoja asaini bondi ya Sh milioni 10, Melo alitimiza masharti hayo na kuachwa kwa dhamana.

Baada ya kuachwa, alikamatwa na kupandishwa tena kwa Hakimu Nongwa, ambaye alitaka mshitakiwa awe na wadhamini wawili, wasaini bondi ya Sh milioni moja kila mmoja, au ajidhamini kwa kusaini bondi hiyo.

Alipotoka hapo, alipandishwa kwa Hakimu Mwambapa, ambaye alitaka mshitakiwa awe na wadhamini wawili, wasaini bondi ya Sh milioni tano kila mmoja, ambapo Melo alishindwa masharti hayo na kujikuta akirudishwa mahabusu.

Kesi hizo ziliahirishwa hadi Desemba 29 zitakapotajwa na kuangalia kama upelelezi umekamilika.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo