Kafulila aigeuka NCCR, arudi Chadema


Celina Mathew

David Kafulila
ALIYEKUWA Mbunge wa Kigoma Kusini, David Kafulila, ameachana na chama cha NCCR-Mageuzi na kurudi Chadema, kwa alichoeleza kuwa ndicho chama kilichojipambanua kuelekea safari ya mabadiliko mwaka 2020.

Kada huyo tayari amewasilisha barua kwa Katibu Mkuu wa NCCR-Mageuzi, Mosena Nyambabe kumjulisha kujivua uanachama na kwamba anakwenda Chadema.

Akizungumza na mwandishi wa JAMBO LEO jana, Kafulila alisema hakufanya uamuzi huo kwa kukurupuka, bali kutokana na kutafakari na kushauriwa na wananchi wa jimbo lake, hivyo ameridhika na Chadema kwa kuwa ndiyo sehemu inayojipambanua.

"Nimetafakari na kushauriwa sana jimboni na nimeridhika, kwamba Chadema ndiyo sehemu iliyojipambanua kwa mikakati ya kuleta mabadiliko yanayotarajiwa na Watanzania na ni vema kukusanya nguvu ya kila mwenye kiu ya mabadiliko ndani ya chama kimoja, ili kufupisha safari ya mabadiliko," alisema.

"Leo (jana) nimewasilisha barua kwa Katibu Mkuu wa Chama kumjulisha kwamba nimejivua uanachama na uongozi na nina mpango wa kurejea Chadema," alifafanua Kafulila.

Alipotakiwa kufafanua kuhusu historia ya migogoro na viongozi aliokuwa nao Chadema kabla ya kuhamia NCCR-Mageuzi,  ambapo aliyekuwa Katibu  Mkuu wa Chadema, Dk Wilibrod Slaa alipata kumwita ‘sisimizi’ kwa alichoeleza kukosa imani naye, Kafulila alijibu kuwa siasa ni malengo si uhusiano binafsi.

Aliongeza kuwa wanasiasa wanaunganishwa na malengo zaidi ya urafiki na yeye malengo yake sasa ni kuendelea kupigania mabadiliko ya kimfumo yanayoenea zaidi Chadema kuliko chama kingine.

Historia

Novemba 10, 2009 Kafulila alijivua uanachama Chadema na kuhamia NCCR –Mageuzi, baada ya kuondolewa kwenye nafasi ya Ofisa Habari aliyokuwanayo.

Akiwa NCCR-Mageuzi, alitimuliwa uanachama akidaiwa kukiuka taratibu za chama hicho na tuhuma za kutaka 'kumpindua' Mwenyekiti James Mbatia.

Hata hivyo, suala hilo lilipata suluhu baada ya Mbatia kuteuliwa na Rais mstaafu Jakaya Kikwete kuwa mbunge, na wakiwa bungeni, Mbatia na Kafulila walikutana, kuzungumza na kufikia uamuzi wa kumaliza mzozo uliokuwapo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo