Kiwango cha fedha chapunguza wateja Mahakama ya Mafisadi


Salha Mohamed

Dk Harrison Mwakyembe
SERIKALI imesema itajadili kushusha kiwango cha fedha za makosa ya rushwa na uhujumu uchumi kwenye Mahakama ya Mafisadi ili kukomesha vitendo vya rushwa.

Pia Serikali ya Mkoa wa Dar es Salaam inakusudia kujenga mahakama za mwanzo 20 mwakani kwenye wilaya zote jijini humo lengo likiwa ni kupunguza kesi zinazokaa muda mrefu.

Akizungumza Dar es Salaam jana baada ya kufanya mazungumzo na Mkuu wa Mkoa huo, Paul Makonda, Waziri wa Katiba na Sheria, Harrison Mwakyembe alisema Wizara ilianza mapema kuhakikisha inafanya mabadiliko ya sheria ya kuunda Divesheni Maalumu ya Mahakama ya Mafisadi.

“Waandishi waliuliza tangu Julai hadi sasa kungekuwa na kesi nyingi, lakini kuna kesi moja…tumekuja kubaini kwamba uchache wa kesi ndiyo mafanikio makubwa ya hatua ya kisheria tuliyochukua,” alisema.

Alisema kwa sasa waliozoea kupora mabilioni ya fedha wamerudi nyuma ambapo wameonekana wakiiba fedha chini ya Sh bilioni moja.

“Sisi Serikali tukiona wizi sasa umepungua na kuenea katika viwango vya Sh milioni 400, 500 na 700 tumeanza kujadiliana kuangalia uwezekano wa kushusha kiwango cha fedha, ili kukomesha udokozi, ubadhirifu, wizi wa fedha au mali ya umma,” alisema.

Mwakyembe alisema katika mwaka mmoja, wamepitisha sheria ya kulinda watoa taarifa na mashahidi, ili kuiwezesha divisheni ya hiyo na wapelelezi kupata ushahidi wa kutosha.

Alifafanua uamuzi wa Mkuu wa Mkoa huo, Paul Makonda kutafuta vijana wanaojua sheria ili kusaidia wananchi kabla ya kwenda mahakamani kuwa ni mzuri.

“Sisi tayari tumepeleka Muswada wa Msaada wa Kisheria ambao utasaidia wananchi hasa wa vijijini na wanawake ambao ndio wanaumizwa na desturi zilizopitwa na muda,” alisema.

Alisema kuanza kwa sheria hiyo kuitafanya kuwa na wasaidizi wa kisheria nchi nzima wapatao 4,900. ”Naupongeza mkoa kuwa wa kwanza vijana kuanza kazi na baada ya muda mtakuwa walimu wa kwanza kwa hili suala,” alisema.

Alisema bado kuna tatizo wanalopaswa kuliangalia kwa pamoja ambalo ni nidhamu na maadili ya watendaji ndani ya Mahakama. 

Makonda alisema walijadili utoaji na upatikanaji wa haki kwa wakati, kwani kuna changamoto ya watu kuwa wengi na kuchelewa kupata haki zao.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo