Zika yaumiza kichwa

*Waziri akanusha ugonjwa huo kuingia nchini
*Naibu wake atoa mwito wananchi wajikinge

Waandishi Wetu

WAKATI Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu akisema ugonjwa wa zika haujaingia, nchini, Naibu wake Dk Khamis Kigwangalla ametaka wananchi wajikinge nao kama wafanyavyo kwa malaria.

Hata hivyo, Mwalimu aliwataka wananchi kuondoa hofu ya ugonjwa huo kwa vile haujathibishwa kuwapo nchini.

Waziri katika taarifa yake jana, alisema utafiti wa Taasisi ya Taifa ya Utafiti wa Magonjwa ya Binadamu (NIMR) na matokeo yake kutangazwa juzi, ulihusu kuchunguza ubora wa kipimo kipya cha magonjwa ya zika na chikungunya.

Mwalimu alisema hayo alipokuwa akitoa ufafanuzi wa taarifa ya utafiti ya zika nchini kwa waandishi wa habari Dar es Salaam.

Alisema utafiti uliofanywa na NMRI kitaifa ni hatua za awali za kuangalia ubora wa kipimo, hivyo matokeo hayo yanapaswa kuchunguzwa kwa kina kupitia vipimo vilivyothibishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO).

“Wizara yangu itashirikiana na taasisi za ndani na nje ya nchi, kuendeleza utafiti na ufuatiliaji wa kitaalamu, ili kuzuia ugonjwa huo kuingia nchini,” alisema.

Alisema sekta ya afya ina utaratibu wa kutoa taarifa ya magonjwa ya kuambukiza ambayo ni hatari, ikiwamo zika, ebola na mengineyo, hivyo mikakati ya ufuatiliaji wa zika imeandaliwa na taarifa itatolewa.

Mkurugenzi Mkuu wa NIMR, Dk Mwele Malecela alisema taasisi hiyo ilifanya utafiti wa ubora wa kipimo kipya, ili kujiridhisha kama kina uwezo wa kupima virusi vya zika.

“Taarifa yangu ilitoa matokeo ya virusi vya zika vinavyoweza kusababisha watoto kuzaliwa na kichwa kidogo, haikumaanisha kuwepo kwa ugonjwa huo, tunafahamu Wizara ndiyo yenye dhamana ya kutangaza,” alisema.

Mganga Mkuu wa Serikali, Profesa Mohammed Bakari alisema wataalamu wataendelea kuzifanyia uchunguzi taarifa za NIMR ili kujiridhisha.

“Wataalamu wakikamilisha uchunguzi wa taarifa, utaratibu utaandaliwa baada ya kujiridhisha, lakini hivi sasa Mamlaka haijajiridhisha kwa vile ni taarifa za awali,” alisema.

Dk Kingwangwala alitaka wananchi waondoe hofu, kwani hakuna tofauti ya kujikinga zika na malaria.

“Tunapaswa kutumia vyandarua kuzuia mbu na kutunza mazingira, huku Serikali ikiendelea kuchunguza taarifa za awali za NIMR, ili kutoa taarifa rasmi,” alisema.

Juzi Dk Mwele alikutana na waandishi wa habari kueleza ripoti ya utafiti wao ikionesha zika kuwapo nchini na kuendelea na utafiti kujua ukubwa wa tatizo.

Utafiti huo ulifanyika kati ya mwaka jana na mwaka huu katika mikoa minane na jumla ya sampuli 533 za damu zilipimwa na kati yao, watoto wachanga 80 walizaliwa na ulemavu wa viungo.

Baada ya utafiti walibaini kuwa asilimia 43.8 ya watoto wachanga waliambukizwa virusi vya zika.

Mikoa iliyofanyiwa utafiti ni Mwanza, Simiyu, Shinyanga, Geita, Kigoma, Tabora, Singida na Morogoro, na bado taasisi hiyo na Chuo Kikuu cha Bugando, Mwanza wanaendelea na utafiti ili kujua ukubwa wa tatizo hilo kwenye mikoa hiyo.

Dk Mwele alitoa taarifa hiyo wakati akielezea mafanikio ya taasisi yake kwa mwaka mmoja na kusema kati ya watu 533 waliopimwa, 83 (asilimia 15.6) waligundulika kuwa na maambukizi ya virusi vya zika na hivyo kupewa matibabu haraka.

“Kwa wale watoto wachanga 80 waliozaliwa na ulemavu, asilimia 43.8 walikuwa wameambukizwa virusi vya zika na hadi sasa bado tunaendelea na utafiti kubaini ukubwa wa tatizo hili na kuchukua hatua za haraka,” alisema Dk Mwele.

Leonce Zimbandu na Jemah Makamba


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo