Wingu zito lagubika Wizara



FARU JOHN
 
*Maelezo ya wakurugenzi yajikanganya, yashindwa kujibu maswali ya msingi
*Wao wadai faru John alikuwa mkorofi, alizaa na watoto na wajukuu zake

Celina Mathew

WAKATI mwaka ukienda ukingoni, sakata la kupotea kwa faru John limegubikwa na wingu zito baada ya baadhi ya vigogo wa Wizara ya Maliasili na Utalii kushindwa kutoa majibu sahihi zaidi ya kujikanganya kwenye maelezo yao.

Hali hiyo imeendelea kuibua maswali bila majibu ingawa tayari Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa ameunda tume ya kuchunguza utata wa faru John.

Wakati tume hiyo ikiendelea kuchunguza sakata hilo, jana baadhi ya vigogo wa Wizara hiyo walizungumzia kifo cha faru huyo huku wakishindwa kueleza alikufa lini na kwa ugonjwa gani na wapi alipelekwa.

Mkurugenzi Msaidizi wa Uendelezaji wa Wanyamapori, Dk Nebbo Mwina na Mkurugenzi wa Idara ya Sera na Mipango, Dk Idd Mfunda walitoa ufafanuzi kuhusu faru John huku wakitofautiana na kushindwa kutoa majibu sahihi.

Hali hiyo ilizusha maswali ya wadau waliokuwa wakuifuatilia maelezo ya vigogo hao hata walipoulizwa swali la aina moja kuhusu faru huyo majibu yao yalitofautiana.

Wakizungumza kwenye kipindi cha Tuongee Asubuhi kinachorushwa na luninga ya Star TV wakurugenzi hao walisema wanatambua tume iliyoundwa kuchunguza utata wa faru huyo.

Moja ya maswali waliyoulizwa ni kuhusu sababu za faru John kuhamishwa kutoka Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro, ambapo Dk Mwina alijibu kuwa ilitokana na tabia yake ya kupiga wenzake na kuzaa na ndugu zake.

Faru huyo badala ya kuhamishiwa kwenye hifadhi nyingine ya Taifa alipelekwa kwa mtu binafsi (Grumeti) huku Dk Mwina akisema alipelekwa Grumeti akazalishe faru wengine kwani huko kulikuwa na faru jike.

Dk Mwina alisema kwa kuhamishiwa Grumeti waliamini faru John asingefanya aliyokuwa akifanya Ngorongoro. “Angekwenda Serengeti angesababisha athari mbaya kama za Ngorongoro; kuzaa na ndugu zake na vurugu za kupiga wenzake."

Alifafanua kuwa Grumeti hawakulipa fedha kwa kuwa faru John alikuwa chini ya Wizara na alikuwa hauzwi bali kilicholipwa ni gharama za kumsafirisha na kushindwa kueleza ni kiasi gani kilitumika.

Walipoulizwa kwa nini hawakumpeleka Serengeti ambako walimwomba, Dk Mwina alisema Grumeti ni wadau wao kwa kuwa walikuwa wanaleta faru kutoka Uingereza, na faru dume waliyekuwa naye alikufa hivyo kumwomba John.

Kuhusu kufa kwa faru John, Dk Mfunda alikiri kuwa kweli alikufa na kuhusu kaburi lake alijibu hakuzikwa lakini pia hakuweza kujibu kuhusu kiini cha kifo akisema hajui ugonjwa uliomuua.

Hata hivyo, wakati Dk Mwina akieleza kuwa John alikufa Oktoba 10 mwaka jana, wachambuzi wengine kwenye kipindi hicho walimkosoa kwa kumwambia kuwa alikufa Oktoba mwaka huu.

Kwa mujibu wa taarifa, wakati John akiwa hifadhini waajiriwa tisa walikuwa walilipwa Sh 25,000 kila mmoja kumlinda kwa siku, suala ambalo lilihojiwa sababu ya malipo wakati ni waajiriwa, Dk Mwina alijibu kuwa ilikuiwa ni posho ya chakula.

Kuhusu pembe za John, Dk Mwina alisema zilikatwa ili kupunguza makali yaliyokuwa yanasababisha vifo vya wenzake. Hata hivyo, taarifa hiyo ilitofautiana na aliyopewa Waziri Mkuu kuwa pembe zake zilikatika wakati anapigana.

"Hatuwezi kuanika hadharani vitu vinavyochunguzwa.Tuache tume ifanye kazi yake, kisha watoe taarifa sahihi na hata sisi tunazo taarifa, lakini hatuwezi kuzitoa zote kwa sasa," alisema.

Wakati Dk Mwina akitoa maelezo hayo, Dk Mfunda alisema pembe hizo zina biashara, lakini haifanyiki Tanzania bali wanaojihusisha nayo ni wafanyabishara haramu.

Pia alisema pembe za John tayari zilikabidhiwa kwa Waziri Mkuu na alishatoa maelekezo, kwamba hata baada ya kifo cha faru huyo pembe zake zilichukuliwa na kuhifadhiwa ingawa hakumbuki ulikuwa mwezi gani.

Kwenye maelezo ya vigogo hao, kuna wakati walijibu kuwa hawakumbuki na hawajui chochote kuhusu John hali ambayo ilimfanya mwongoza kipindi kuwauliza walichofuata kwenye kipindi wakati walidai kwenda kutoa ufafanuzi na kuweka mambo hadharani.

Wachambuzi

Wachambuzi waliokuwa kwenye kipindi hicho akiwamo mchambuzi wa siasa na uchumi, Herbert Faustine na mchambuzi wa masuala ya kijamii, Cyprian Musiba walisema majibu ya wakurugenzi hao ni vema Rais John Magufuli akayafanyia kazi kwani inaonekana wazi wapo wahusika wa moja kwa moja.

Faustine alionesha kushangazwa na hatua ya baadhi ya watendaji wa Wizara hiyo kujikanganya wakati wakijibu maswali hayo na kueleza kuwa takwimu ni mali ya Watanzania hivyo hawakupaswa kuzificha.

"Majibu yaliyotolewa na baadhi ya watendaji hao wa wizara inabidi kuchunguzwa na Takukuru (Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa) kwani yanadhihirisha ukweli kuhusu faru John.

"Maliasili hakuna ‘jipu’ bali ni ‘saratani’. Hivyo ni vema ikaondolewa, kwa kuwa wanashindwa kueleza ukweli kuhusu sakata hilo," alisema.

Alitumia nafasi hiyo kueleza kuwa ni maumivu kwa Taifa endapo suala hilo litafumbiwa macho, huku akishauri kuwa umefika wakati wizara hiyo ufumuliwe na wahusika wachukuliwe hatua kali.

Musiba alimshauri Waziri Mkuu kuondoa wahusika wote kwani suala kama hilo la kupotea kwa faru liliwahi kutokea mwaka 1992 baada ya kupotea kwa faru mwingine.

"Wizara ile si ya kuchezea, inabidi vikosi vya ulinzi na usalama viende kwenye hifadhi viachane na wananchi. Pia wawepo maofisa wa usalama wa Taifa ili kufuatilia mambo yanavyokwenda kwenye hifadhi na mbuga zetu za wanyama," alisema Musiba.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo