Mabasi ya mwendo wa haraka yakabiliwa na uhaba wa tiketi


Abraham Ntambara

MTENDAJI Mkuu wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART), Leonard Lwakatare ameshindwa kujua ni lini wataongeza kadi nyingine za kielekroniki kwa ajili ya abiria wa mabasi yaendayo kasi, ambazo zitaondoa kero ya chenji na foleni wakati wa kukata tiketi.

Akizungumza na JAMBO LEO jana Dar es Salaam Lwakatare alisema kama Serikali inawajibika kutatua kero hizo kwa kuhakikisha tiketi zinapatikana na kubainisha kwamba mchakato unafanyika kupitia mfumo wa Sheria ya Manunuzi ya Umma.

“Mfumo wa Manunuzi ya Umma siyo wa haraka, unahitaji kufuata utaratibu, sasa naogopa kusema ni lini suala hili litakamilaka kwa sababu ni mchakato, lakini tupo kwenye utaratibu wa kupata hizo kadi,” alisema Lwakatare.

Aidha alisema wamepiga hatua zaidi katika kuhakikisha wanalimaliza suala hilo. Alibainisha kuwa, mategemeo yao ni kwamba zikipatikana tu wataanza kuziuza kwa abiria ili zitumike.

Lwakatare aliongeza kuwa tayari walishaitisha tenda ya kupata mtu ambaye atalishughulikia suala hilo na kusisitiza kuwa mchakato huo uko katika hatua nzuri.

Alibainisha kama michakato yote ingekuwa imekamilika kwa kuingia mikataba na kila kitu kuwa sawa ndiyo angeweza kujua na kusema lini kadi hizo zitakuwa tayari kwa matumizi.

Mtendaji huyo alisema katika kuhakikisha wanasaidia kutatua changamoto ya chenji kwa dharula wao pia wanafanya juhudi kuhakikisha chenji zinapatikana kwenye vituo vya mabasi yaendayo kasi.

Alisema juhudi hizo zinafanyika kwa kwenda kuomba chenji hizo kwenye benki ili kuhakikisha kuna kuwa na chenji za kutosha na kuzisambaza kwenye vituo vyote.

Lwakatare alisisitiza kuwa ni haki ya kila mtu kupata chenji yake bila kubaguliwa, hata kwa yule anayekuja na sh. 10000 ambapo alibainisha kuwa ni kazi ya muuza tiketi kurudisha chenji.

Alisesitiza kuwa ni wajibu wa mtu anayeuza tiketi kuhakikisha anakuwa na chenji za kutosha ili kuwarudishia abiria bila kuwabagua ilimladi mtu anahitaji chenji yake.


Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo