Mwekezaji Epanko ahaha kusaka suluhu


Suleiman Msuya

MGOGORO wa baadhi ya wakazi wa kijiji cha Epanko kilichoko Kata ya Nawenge wilayani Ulanga na mwekezaji wa kampuni ya TanzGraphite (TZ) Limited, unaelekea ukingoni, baada ya kampuni hiyo kueleza kuwa inajipanga kulipa fidia kwa wakazi 388 watakaoathirika na uwekezaji huo ifikapo mwakani.

Msemaji wa kampuni hiyo, Nassor Said, alitaja mali zitakazolipwa fidia kuwa ni pamoja na nyumba, mashamba na makaburi.

Alisema pamoja na kulipa fidia hiyo kampuni pia itatekeleza madai mengine kadhaa ya wananchi hao, ikiwamo ujenzi wa kiwanja cha mpira, zahanati na wazee kukatiwa bima ya afya jambo ambalo pia wamekubali kutekeleza.

“Ninachokiona hapa ni wananchi wa Epanko wanahitaji elimu zaidi hasa kundi la wachache ambao kila kikucha wanaibuka na kulalamika,” alisema.

Said alibainisha kuwa hakuna uchimbaji ambao utaanza bila hatua zote muhimu kukamilika, hivyo hakuna sababu ya wananchi kuwa na hofu na mradi huo.

Mgogoro

Hivi karibuni wakazi wa kijiji cha Epanko, walijitokeza na kubainisha kuwa wamekuwa wakipatiwa vitisho kutoka kwa mwekezaji huyo na Serikali, hali ambayo imewafanya waishi kwa hofu.

“Ni takribani mwaka mmoja tunaishi kwa shida sana kwani sisi unatuona hapa tunashindwa kurejea kijiji kwetu kwa kuhofia kukamatwa, kwani wenzetu wawili wamekamatwa na polisi kutokana na agizo la Mkuu wa Mkoa Dk. Kebwe Steven,” alisema mmoja wa wakazi hao.

Alieleza kuwa mgogoro uliopo unatokana na mwekezaji huyo kushindwa kufuata taratibu za uwekezaji kama Sheria ya Madini ya 2010.

Diwani

Akizungumzia sakata hilo Diwani wa Kata ya Newenge ambapo kijiji hicho kipo Protas Lukombe, alisema mgogoro huo ulikuwepo ila kwa sasa umeanza kutatuliwa.

Diwani huyo alisema mwanzoni alikuwa na kundi hilo ambalo linatetea maslahi ya wananchi na kuandika barua kwenda kwa waziri mkuu, ila baada ya kupata elimu kuhusu suala hilo yupo tayari kuhama na kuachia wawekezaji hao.

Mwenyekiti CCM

Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Wilaya ya Ulanga, Khalid Naloto alisema mgogoro huo upo kwa muda na anaufahamu, lakini anavyojua, kuna juhudi zinafanyika kutatua.

Alisema kamati ya siasa ya wilaya inatarajia kufanya ziara Desemba 21 na 22 katika kijiji cha Epanko ili kuweza kupata muafaka wa suala hilo kwa wakati na wananchi kuendelea na shughuli zao.

“Naomba unipe nafasi nalifanyia kazi sualah ilo kwani ni suala ambalo linahitaji kupata taarifa kamili,” alisema.

RPC

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Morogoro, Ulrich Matei, alisema mgogoro huo anaujua na kuwa kukamatwa kwa watu wawili katika kikao cha mkuu wa mkoa kulitokana na kutoka lugha chafu na kwamba kutopakupata dhamana ni jukumu la mahakama.

Matei alitoa wito kwa watu wote ambao wana matatizo kutoa taarifa kwa jeshi hilo na kwamba wao hawapo tayari kuona mtu akionewa kwani kila mwananchi ana haki.

“Pamoja na mambo mengine nawashauri wananchi wa Ipango kufuata taratibu kwa kusshirikisha viongozi wa husika katika mgogoro huo lakini pia mbunge wao yupo wamtumie,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo