Guninita amng’ang’ania Nape, Mgeja amsamehe


Charles James

John Guninita
ALIYEKUWA Mwenyekiti wa CCM wa Mkoa wa Dar es Salaam, ambaye sasa yuko Chadema, John Guninita, amekataa kumsamehe aliyekuwa Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa (Nec) ya CCM, Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye.

Guninita alifikia hatua hiyo jana alipoulizwa na mwandishi wa habari hizi, kueleza msimamo wake baada ya Nape kuomba msamaha kwa wanasiasa na viongozi wa vyama vya Upinzani kwa kauli zake alizopata kuzitoa, huku akimtuhumu Waziri huyo wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo kuwa ni mnafiki.

Tofauti na msimamo wa Guninita, kada mwingine wa zamani wa CCM, Khamis Mgeja ambaye alikuwa Mwenyekiti wa CCM mkoani Shinyanga, naye sasa kuwa Chadema, alisema kilichofanywa na Nape ni kitendo cha kiungwana.

Nape aliomba msamaha huo wakati akimkabidhi ofisi, mrithi wake, Humphrey Polepole, aliyeteuliwa na NEC kushika nafasi hiyo katika mabadiliko ya ndani ya chama yaliyofanywa mapema wiki hii.

Guninita alisisitiza kuwa msamaha ulioombwa na Nape kwa wapinzani ni wa kinafiki, kwa sababu alitoa kauli hizo akiwa kwenye majukumu ya chama chake, hivyo msamaha huo alipaswa kuomba wanachama wenzake ndani ya CCM.

Alisema Nape alikuwa na haki ya kuomba radhi wanasiasa ndani ya chama chake, kwa sababu ndio anaendelea kushirikiana nao katika majukumu ya chama chao, huku akisema ataendelea kupambana na wapinzani kwenye majukwaa ya kisiasa, hivyo msamaha huo ni sawa na bure, kwani bado ataendelea kukumbana nao kutokana na kuwa na misimamo tofauti kiitikadi.

“Unajua, kwenye siasa mtu unapotoa matamko yoyote hasa ukiwa kwenye nafasi kama aliyokuwa nayo yeye, ujue uko kazini na unafanya kazi uliyotumwa na chama, hivyo kuomba msamaha ni sawa na kuonesha unafiki kisiasa,” alisema Guninita.

Akizungumzia kauli zilizowahi kumkera na kuumiza wapinzani kuwa ni pamoja na ile ya ‘goli la mkono’, ‘wapinzani ni majitaka’, na ya kuwaita waliojitoa CCM kwenda Upinzani kuwa ‘makapi’ huku akisema zilikosa busara na uungwana.

Mgeja

Hata hivyo, Mgeja alifafanua kuwa kilichofanywa na Nape hata kwenye vitabu vya dini imeandikwa, kuwa mtu anapokosea, anapaswa kuomba radhi huku akisema atamkumbuka kwa kauli zake za kuudhi wapinzani, ikiwamo aliyotoa wakati wa Uchaguzi Mkuu mwaka jana kuwa ‘CCM itashinda hata kwa bao la mkono’.

“Nape bado ni kijana mdogo na pengine kauli alizokuwa akitoa zilitokana na utoto na kulewa madaraka, hivyo kama ameamua kuomba msamaha ni wazi ameonesha kukua kisiasa na anapaswa kupongezwa na kusamehewa,” alisema Mgeja.

Wawili hao walijiondoa CCM na kujiunga na Chadema Agosti 13 mwaka jana, baada ya walichokieleza kuwa ni kutoridhishwa na mwenendo wa chama hicho kwenye mchakato wa kupata mgombea urais.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo