Faru John sasa ‘kufa’ na vigogo


*Wasomi wasema ung’ang’anizi wa Majaliwa una kishindo
*Wasema ameshanusa kitu anatafuta uhakika kukimaliza

 Waandishi Wetu

Kassim Majaliwa
ANAUJUA ukweli. Ndivyo wanavyoeleza wanasiasa na wasomi waliozungumza na gazeti hili kuhusu uamuzi wa Waziri Mkuu, Kassim Majaliwa, kuunda timu mpya ya kuchunguza mazingira ya kifo cha faru John, kubainisha kuwa mnyama huyo atang’oka na vigogo wa Wizara ya Maliasili na Utalii.

Wakizungumza na JAMBO LEO kwa nyakati tofauti, walisema kitendo cha Mtendaji Mkuu huyo wa Serikali kutaka kaburi la faru huyo kufukuliwa ili kuchukuliwa vinasaba vya mwili wake na kuvilinganisha na vya ndama wake na pembe zake wakati wa kuwasilishwa kwa taarifa ya kifo na kuhamishwa kwake kutoka hifadhi ya Sasakwa kwenda Grumeti, kinaonesha kuwa lazima ukweli idhihiri na hatua zichukuliwe dhidi ya ubadhirifu kama ulikuwapo.

“Waziri Mkuu ana taarifa zote na huenda zikawa kinyume na alichoelezwa na watendaji wa mamlaka za maliasili na utalii, akiwamo Maghembe (Profesa Jumanne-Waziri). Anachokifanya ni kujiridhisha tu na kufuata sheria na taratibu kabla ya kuchukua hatua,” alisema Dk George Kahangwa, Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wanataaluma wa Chuo Kikuu Dar es Salaam (Udassa).

Desemba 6 akiwa Arusha Waziri Mkuu Majaliwa aliagiza uongozi wa Mamlaka ya Hifadhi ya Ngorongoro (NCAA), kumpa nyaraka zote zenye taarifa za kumhamisha faru Desemba 8 huku taarifa iliyotolewa na Profesa Maghembe, ikisema mnyama huyo alihamishwa kutoka Sasakwa na kupelekwa Grumeti, Desemba mwaka jana.

Katika maelezo yake, Waziri Maghembe alisema uamuzi wa kumwondoa ulikuwa muhimu ili kuongeza idadi ya faru weusi na kupunguza tatizo la ‘inbreeding’ ndani ya Ngorongoro, na kwamba faru huyo alikufa Agosti 18.

Kitendo cha Waziri Mkuu Majaliwa kukabidhiwa pembe hizo na kuendelea kuwa na wasiwasi na taarifa alizopewa kama alivyoagiza huku akitaka  aoneshwe kaburi, zimeibua wasomi hao na kubainisha kuwa haihitajiki shahada kutambua kuwa kuna kitu kimebainika tayari.

Katika maelezo yake, Dk Kahangwa alisema Waziri Mkuu alitumia falsafa ya kutomwamini mtu yeyote, kwamba iwapo uchunguzi huo utatoa majibu tofauti na taarifa zilizotolewa na Wizara ya Maliasili na Utalii, lazima kuna watakaowajibika.

Kauli hiyo iliungwa mkono na Mhadhiri mwingine wa Chuo hicho Richard Mbunda, aliyesema “anataka kufuatilia jambo hili hadi mwisho. Ni mfano kwa watendaji wengine wa Serikali wanaoachia mambo njiani. Sioni lililojificha kwa wahusika wa faru huyo, ila kitendo cha Waziri Mkuu kutoridhika, tafsiri yake ni kuwa kuna jambo limejificha. Ukweli tutaujua tu ngoja uchunguzi ukamilike.”

Alisema sakata hilo limeibuka kipindi ambacho nchi imekuwa na matukio mengi ya ujangili, huku akitolea mfano wa kashfa ya kusafirishwa kwa twiga na ngedere kupitia Uwanja wa Kimataifa wa Ndege wa Kilimanjaro (KIA), “Serikali ya Awamu ya Tano inataka kuonesha utofauti wake na awamu iliyopita.”

Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk Benson Bana alisema: “Anajua kiundani jambo hili na anachokifanya ni  kuonesha  kuwa yeye ni mtu anayefuata sheria. Ameunda tume, akiamini baada ya majibu atakuwa katika nafasi muhimu ya kufanya uamuzi na huenda tukashuhudia watu wakitumbuliwa.”

Dk Onesmo Kyauke pia wa UDSM aliungana na Dk Bana huku akienda mbali zaidi akisema mpaka suala hilo linafika kwa Waziri Mkuu ni wazi kuwa Waziri mwenye dhamana alishindwa kulishughulikia.

“Kama ni kweli faru huyo hajafa bali alitoroshwa au kuuzwa, ni lazima mtu atatumbuliwa tu sambamba na watendaji wengine. Faru wapo wachache nchini, lazima Serikali iwe macho kuhakikisha hawapotei,” alisema.

“Unaweza ukajiuliza Maghembe alishindwa vipi kulimaliza suala hili? Ni jambo linalofikirisha sana, lina maswali zaidi kuliko majibu,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo