Kesi 10 zilizotikisa 2016


*Wamo Lissu, Lipumba, waliokuwa vigogo TRA

Grace Gurisha

WAKATI mwaka 2016 ukielekea ukingoni, Watanzania wanakumbuka kesi kumi kubwa zilizotikisa mwaka huu wa kwanza wa utawala wa Rais John Magufuli.

Uchunguzi umebaini kuwa Watanzania wengi hasa wa mijini, wamejadili kesi ya aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Harry Kitilya na wenzake na kesi ya aliyekuwa Kamishna wa Forodha na Ushuru wa Mamlaka ya Mapato (TRA), Tiagi Masamaki na wenzake.

Kesi zingine zilizovuta hisia za watu wengi mwaka huu ni Mpemba wa Magufuli (Yusuf Yusuf), mwanzilishi wa mtandao wa Jamii Forums, Maxence Melo, mfanyabiashara bilionea aliyetajwa na Rais Magufuli kuwa anajipatia fedha kati ya Sh milioni saba kwa dakika moja, Mohamed Yusufali ambaye alipandishwa kizimbani kwa makosa ya kuisababishia Serikali hasara ya zaidi ya bilioni 14.

Pia, mwaka huu kulikuwa na kesi ya aliyekuwa Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Vitambulisho (Nida), Dickson Maimu, Profesa Lipumba na Maalim Seif, kesi ya uchochezi inayomkabili Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu, kesi ya aliyekuwa Mkurugenzi Mtendaji Kipallo Kisamfu wa Kampuni ya Reli Tanzania (TRL) ‘mabehewa feki’, kesi ya wabunge wa CCM kizimbani kwa rushwa na Zombe kufutiwa kesi ya mauaji.

Kesi Kitilya

Kitilya na wenzake walipandishwa kizimbani katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam wakishitakiwa kwa makosa la Uhujumu Uchumi, likiwemo la kutakatisha fedha haramu na kujipatia isivyo halali dola za Marekani milioni 6, sawa na sh bilioni 12.

Mawakili wake walipigana kufa na kupona ili mteja wao aondolewe kosa la kutakatisha fedha, lakini ilishindikana, baada ya Mahakama Kuu Kanda ya Dar es Salaam kutoa uamuzi kuwa shitaka hilo liko kihalali katika hati ya mashitaka.

Kutokana na hali hiyo Kitilya bado anaendelea kusota rumande kwa sababu upelelezi wa kesi hiyo bado haujakamilika.

Kesi ya Masamaki

Kesi ya Masamaki maarufu kama kesi ya makontena ilitikisa nchi kutokana na taarifa ambazo zilikuwa zinazagaa kuwa tajiri huyo ana nyumba zaidi ya 70 na pia ndani ya nyumba yake aliyokuwa akiishi, alikutwa na mabilioni ya fedha.

Hata hivyo, Masamaki na wenzake waliachiwa kwa dhamana na Mahakama Kuu, baada ya kutimiza masharti waliyopewa. Bosi huyo huyo yupo nje na upelelezi wa kesi yake bado haujakamilika.

Mpemba wa Magufuli

Yusuf Yusuf maarufu kwa jina la Mpemba, alipandishwa kizimbani, baada ya Rais Magufuli kumtaja hadharani kuwa ni kinara wa ujangili wa kujihusisha na biashara ya meno ya tembo. Mwenyewe amekana kosa na upelelezi wa kesi yake bado haijakamilika.

Bilionea Yusufali

Mfanyabiashara bilionea aliyetajwa na Rais Magufuli kuwa anajipatia fedha kati ya Sh milioni saba kwa dakika moja, Mohamed Yusufali alipandishwa kizimbani kwa tuhuma za kuisabishia Serikali hasara ya Sh bilioni 15 kwa kukwepa kodi.

Yusufali bado anaendelea kusota rumande kwa sababu upelelezi wa kesi hiyo haujakamilika kutokana na kwamba katika makosa 199 yanayomkabili, moja ni la kutakatisha fedha haramu ambalo kisheria halina dhamana.

Maimu

Siku chache tu baada ya Rais Magufuli kueleza uchafu uliyoko ndani ya Nida, Mkurugenzi wa Mashitaka aliwaandalia mashitaka Maimu na wenzake, akituhumu kuisababishia serikali hasara ya zaidi ya Sh bilioni moja kwa kutumia mamlaka yao vibaya.

Kesi hiyo imeanza kusikilizwa, baada ya upelelezi wake kuchukua muda mrefu kukamilika.

Profesa Lipumba na Maalim Seif

Bodi ya Wadhamini ya Chama cha Wananchi (CUF) kilifungua kesi katika Mahakama Kuu dhidi ya Lipumba na wenzake na kuiomba Mahakama hiyo itengue barua ya Msajili wa Vyama vya Siasa, Jaji Francis Mutungi iliyomtambua Lipumba kuwa mwenyekiti wa chama hicho.

Watu wengi wanataka kujua mwisho wa kesi hiyo kutokana na nguvu ya Profesa Lipumba katika siasa za upinzania. Kesi hiyo ipo katika hatua ya kuanza kusikilizwa.

Zombe huru, Bageni kunyongwa

Kuachiwa huru kwa aliyekuwa Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa wa Dar es Salaam (RCO) Kamishna Msaidizi wa Polisi (ACP), Abdallah Zombe kulizua maswali mengi sana kwa Watanzania wengi kutokana na kwamba tayari wao walishamuhukumu kutokana na sifa ambazo alikuwa nazo.

Wengine walifikia hatua kusema anatumia nguvu za giza kutokana na hukumu ambayo ilitolewa ya yeye kuachiwa na aliyekuwa bosi wa Jeshi la Polisi, Christopher Bageni kuhukumiwa kunyongwa hadi kufa.

Kesi hii ilikuwa inawasimumua watu wengi kutokana na umaarufu wa Zombe katika kazi ya Jeshi la Polisi aliyokuwa akifanya, kwa hiyo watu walitegemea Zombe ndiyo atafungwa na sio Bageni kwa sababu Bageni alikuwa anafuata maagizo ya bosi wake.

Kisamfu

Kisamfu alipandishwa kizimbani na vigogo wengine 10 akituhumiwa kutumia vibaya madaraka yake kwa kushindwa kusimamia vizuri zabuni kama ilivyokuwa inatakiwa kwenye vigezo vya masharti na kusababisha kununuliwa kwa mabehewa 25 ambayo hayana ubora.

Kesi hiyo ilipelekwa mahakamani baada ya Waziri husika kupiga kelele baada ya kubaini kuwa mabehewa hayo yalikuwa chini ya kiwango.

Melo

Kesi ya kushindwa kulisaidia Jeshi la Polisi katika kutekeleza majukumu ya upelelezi inayomkabili Melo ilizua utata mkubwa katika tasnia ya habari kutokana na kwamba alikuwa akishinikizwa kutoa taarifa za kieletroniki ambazo zilikuwepo kwenye mtandao wa Jamii Forums ambao anaouendesha.

Hali hiyo ilisababisha Melo kukaa mahabusu zaidi ya siku tano, kitu ambacho kilisababisha hofu kwa watu wengi ambao walikuwa wanachangia katika mtandao huo wa kijamii.

Baadaye Melo aliachiwa kwa dhamana na Mahakama ya Hakimu Makazim Kisutu, Dar es Salaam, baada ya kukaa mahabusu siku sita akishikiliwa na Jeshi la Polisi kwa mahojiano.

Lissu

Lissu alipandishwa mara tatu kizimbani akituhumiwa kutoa maneno ya uchochezi, likiwemo la ‘dikteta uchwara’. Jamii imekuwa ikifuatilia kesi hiyo hasa ilipoelezwa kuwa hata pale ambapo alishindwa kutokea mahakamani bila taarifa, mamlaka husika zilishindwa kumkamata, licha ya mahakama kutoa hati ya kumkamata.

Hali hiyo ilizidi kumpaisha Lissu katika kesi zake, ambapo kila mtu alitamani kujua kinachofuata. Kesi hizo zimeanza kusikilizwa, huku Mbunge huyo akionekana kujiamini.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo