Mgeja amuombea msamaha Lowassa


Hastin Liumba, Tabora
Edward Lowassa


KADA wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Khamis Mgeja amewaomba Watanzania kumsamehe waziri mkuu wa zamani, Edward Lowassa kwa kushindwa kuwashukuru baada ya uchaguzi mkuu.

Ametaka wajue kuwa kada huyo aliyehamia Chadema baada ya kukatwa jina lake kwenye orodha ya wagombea urais wa CCM, sasa yupo kwenye kifungo cha kisiasa kutokana na Serikali kuzuia mikutano ya hadhara.

Mgeja alitoa kauli hiyo jana katika Kata ya Tumbi Manispaa ya Tabora wakati alipokuwa akiongea na wanachama na viongozi mbalimbali wa Chadema, pamoja na wananchi wachache waliovamia kikao.

Mgeja alisema anasikitishwa na kitendo cha Lowassa kuzuiwa kuwashukuru wananchi waliompigia kura kupitia mikutano ya hadhara na bado anaamini kuwa hawakumtendea haki.

“Nawaombeni ndugu zangu Watanzania mliopiga kura nyingi na za kishindo kwa mzee wetu Lowassa, kura zaidi ya milioni sita, mtusamehe kwa yeye kushindwa kuwashukuru. Serikali imeminya uhuru wa demokrasia kwa kuzuia mikutano ya hadhara,” alisema.

Alisema Lowassa anapenda sana kuwafikia wananchi kupitia mikutano ya hadhara ili awashukuru kwa heshima kubwa waliyompa, lakini ameshindwa kutokana na mikutano hiyo kuzuiwa.

Hata hivyo, alibainisha kuwa Lowassa hatachoka kuwasemea wananchi hao kero zao na ana imani kero hizo Rais Magufuli na viongozi wa CCM wanazisikia na watazifanyia kazi.

Kada huyo wa Chadema na aliyekuwa Mwenyekiti wa CCM mkoa wa Shinyanga, alisema wananchi wanapaswa kumuelewa Lowassa na Ukawa kwa jumla kuwa wanapenda kufanya mikutano ya hadhara ila wamezuiwa.

Alisema viongozi wanapenda kuwafikia wananchi ili kusikiliza changamoto zao za maisha, pia kuzungumza pamoja kuhusu mustakabali wa nchi, lakini hilo sasa ni gumu kufanyika.

“Sisi wachambuzi wa kisiasa tunaona dhahiri kabisa ishara ya kifungo cha kisiasa kwa Lowassa na viongozi wa vyama vya upinzani nchini. Haya yamefanywa makusudi na watawala ili kuminya demokrasia,” alisema.

Mgeja alieleza kutoridhishwa na tabia aliyosema imeanza kujengeka ya viongozi wa CCM wakiambatana na wakuu wilaya, wakuu wa mikoa na waziri mkuu na Rais kufanya mikutano ya kisiasa ambayo wameizuia kwa wapinzani kwa kisingizio cha misafara ya viongozi wa Serikali.

Hali hiyo ni sawa na kuligawa taifa na siyo rahisi sisi tukae kimya tukishuhudia uvunjwaji huo wa Katiba, alisema.

Mgeja alisema kuwa Tanzania katika ramani ya dunia na Afrika kwa sasa ni nchi ambayo imefanya mambo ya ajabu, kwani watawala wamewahukumu wanasiasa bila kuwasikiliza na hili ni doa kwa taifa.

Alisema kuzuliwa kwa mikutano ya hadhara na kushindwa kutoa ufafanuzi wa kifungu cha kisheria na kikatiba walichotumia kutoa agizo hilo, ni ukandamizaji unaopaswa kukemewa kwa nguvu zote.

Alisema uamuzi unaotolewa na watawala na maelekezo yanayoendelea kutolewa na vyombo vya dola yanakinzana na sheria na Katiba ya nchi.

‘Huu ni ukandamizaji mkubwa uliokubuhu katika demokrasia ya nchi, kwani Tanzania ni nchi iliyokuwa inaheshimika duniani na Afrika, ikiwa mfano wa kuigwa na wengi walikuja kuiga mazuri hapa,” alisema.

Hata hivyo, aliwataka wananchi kuichukulia hali hiyo kama changamoto za kidemokrasi akitolea mfano wa aliyekuwa rais wa Afrika Kusini, Nelson Mandela aliyesema kuwa alifikia hatia kufungwa gerezani kwa sababu ya siasa lakini bado akafanikiwa kuwakomboa wananchi wa Afrika Kusini.

Alisema anaamini ipo siku uhuru wa kweli wa kidemokrasia utapatikana Tanzania kwa njia ya amani kwa kuwa haki haipotei, bali inaweza kucheleweshwa, kwani lisilowezekana kwa binadamu kwa Mungu linawezekana.

Wavamia mkutano

Wakati mkutano huo wa ndani ukiendelea, wananchi
walivamia eneo hilo wakipiga kelele na kudai ‘maji, maji, maji,’ hali ambayo ilimlazimu Lowassa kusimama na kuwatuliza.

Wananchi hao walisikika wakisema hayo, huku wengine wakisema na kuunga mkono ushauri wa Lowassa wa kumtaka Rais Magufuli asitishe ununuzi wa ndege ili ashughulikie kwanza kero ya maji.

Wananchi hao kwa nyakati tofauti walisema wao shida kubwa waliyonayo ni maji, hivyo wakamwomba rais Mafuguli kusitisha mpango wa kununua ndege ili awachimbie kwanza visima vya maji.

Walisema uwezekano wa kuvuta maji kutoka Kahama, Isaka, Ntinde, Nzega, Igunga,Tabora na vikiwemo vitongoji na vijiji hadi Tumbi upo, lakini hakuna nia ya dhati ya kumaliza tatizo hilo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo