Waliokopa elimu ya juu kusakwa nyumba kwa nyumba


Hussein Ndubikile

BODI ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu Nchini (HESLB) imesema kuwa itapita nyumba kwa nyumba, nyumba za ibada na kwenye sherehe kubaini na kuwakamata wadaiwa sugu wa mikopo ambao hawajawasilisha taarifa zao na kurejesha mikopo hadi sasa.

Aidha, Bodi hiyo tangu ilipotoa notisi ya mwezi mmoja imekusanya Sh bilioni 140 kati ya Sh bilioni 300 ilizokuwa ikidai wanufaika wa mikopo.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Dar es Salaam, Mkurugenzi Mtendaji wa Bodi hiyo, Abdul-Razaq Badru alisema tangu notisi itolewe kwa wadaiwa hao na kuongeza wiki mbili, mwitiko umekuwa mkubwa na kuwezesha kiasi kikubwa cha fedha kukusanywa huku ikisisitiza kulazimika kufanya operesheni hiyo kubaini wadaiwa wanaokwepa kurejesha fedha hizo.

"Wiki tatu zilizopita tulitoa ofa kwa wadaiwa, tulianza na wiki nne tukaongeza nyingine mbili, wengi waliojitokeza walirudisha kiasi kikubwa cha mikopo, tunaomba ambao hawajamaliza walipe baada ya muda wa nyongeza wa kulipa, hiari ikimalizika tutapita nyumba hadi nyumba, nyumba za ibada na kwenye sherehe, naamini tutawapata wadaiwa," alisema.

Alisema katika kuhakikisha inatia nguvuni wadaiwa, Bodi itashirikiana na wadau wakiwamo watumishi wake, majirani na idara  na taasisi za Serikali kupata taarifa zao.

Badru alisema baada ya kumalizika muda wa kurejesha kwa hiari, kuanzia Januari mosi bodi itachapisha majina na sura za wadaiwa sugu ili umma uwaone na kuwachukulia hatua za kisheria, ikiwamo kuwakamata na kulazimika kulipa gharama za kuwatafuta.

Alisisitiza kuwa  wadaiwa wa mikopo 42,700 kati ya 142,000 walijitokeza kulipa fedha hizo tangu Bodi itoe notisi ya mwezi mmoja  na kwamba wanufaika walio kwenye mfumo rasmi wa ajira watakatwa asilimia 15 na wasio kwenye mfumo huo watakatwa asilimia 10 ya kipato chao.

Alisema kiwango cha wastani wa makusanyo ya mwezi kimeongezeka kutoka Sh bilioni 2 kwa Januari na Juni Sh bilioni 4 huku Novemba yakiongezeka hadi Sh bilioni 8.

Aliongeza kuwa muda wa kurejesha mikopo kwa wanufaika waliomaliza elimu ya juu uliongezwa kutoka mwaka mmoja hadi miwili baada ya kuhitimu.

Pia alisema Bodi imeunda kikosikazi kitakachokuwa na jukumu la kuwazungukia waajiri ambao hawajaingiza makato ya mikopo ya miaka ya nyuma na wanaoingiza kiasi pungufu cha fedha.

Alifafanua kuwa waajiri walipewa siku 14 kuhakikisha wanawasilisha fedha hizo na taarifa za waajiri walionufaika na mikopo, la sivyo watachukuliwa hatua za kisheria.

Mwanasheria wa Bodi hiyo, Luhano Lupogo alisema makato hayo yalianza kutumika Novemba 18 na kwamba waajiri watakaoshindwa kuwajibika watalipa faini isiyopungua makato hayo au kifungo cha miezi 36 jela.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo