Wasioona waomba elimu ya kilimo


John Banda, Dodoma

KITUO cha watu wenye ulemavu wa macho cha Matembe Bora cha Buigiri wilayani Chamwino ambacho hujishughulisha pia na kilimo cha bustani za mbogamboga, kimeiomba Serikali na taasisi kukipa wataalmu kwa ajili ya elimu itakayowawezesha kuboresha kilimo chao ili kujiinua kiuchumi zaidi na hatimaye waondokane na utegemezi.

Ombi hilo lilitolewa jana na Mwenyekiti wa Kituo hicho, Yarerd Chileso kwa niaba ya wenzake walipopokea msaada wa vifaa vikiwamo nguo, sabuni viatu na mafuta ya kupaka kutoka Umoja wa Madhehebu ya Kikristo Dodoma.

Chileso alisema kutokana na kujishughulisha na kilimo cha mbogamboga kwa lengo la kujiinua kiuchumi wameomba watalaamu hao wa kilimo ili wapate elimu ya kuboresha kilimo na hatimaye kuongeza kipato na kujiinua kiuchumi.

“Sisi tulio hapa kituoni ni walemavu wa macho, lakini pamoja na ulemavu huo tunajishughulisha na kilimo cha mbogamboga kama vile mchicha, kabichi, nyanya, spinachi  na pilipili za kawaida na hoho, lakini hatuna utaalamu, hivyo tunaomba wataalamu ili watuwezeshe kielimu zaidi,” alisema.

Mwenyekiti huyo alisema kilimo hicho pia kimekuwa kikiwawezesha fedha wanazopata kununua mahitaji ikiwa na pamoja kusomesha watoto wao na matibabu.

Aidha, Mwenyekiti huyo alisema kupewa watalamu hao kutawezesha kuachana na tabia ya ombaomba ambayo imekuwa ikifanywa na baadhi ya wasiojiweza kwa kuwa tayari watakuwa wameonesha mfano kwa vituo vingine vinavyotunza wenye mahitaji maalumu ili  kushiriki shughuli za kiuchumi.

Hata hivyo, walemavu hao wakizungumza kwenye hafla hiyo walimtaka Diwani wa Buigiri, Kenneth Yindi kuwasiliana na Serikali ili wawekewe alama za barabarani kutokana na kituo chao kuwa karibu na barabara kuu ya Dodoma - Morogoro ili wavuke kwa usalama zaidi.

Diwani Yindi alisema tatizo la alama za barabarani linatakiwa kushughulikiwa na tayari taarifa zimetolewa kwa kuanzia ngazi ya wilaya hadi Taifa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo