Mbunge kuwasilisha hoja binafsi bungeni


Sharifa Marira

Mohamed Mchengerwa
MBUNGE wa Rufiji, Mohamed Mchengerwa (CCM), amesema atawasilisha bungeni hoja binafsi ya kupendekeza mabaraza ya ardhi yafutwe, kwa sababu yanafanya kazi kinyume cha sheria.

Mchengerwa alisema hayo kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika katika kijiji cha King'ongo, kata ya Muhoro jimboni humo, baada ya wananchi kulalamikia mabaraza hayo kuwakandamiza kwa kugawa ardhi yao kwa zaidi ya miaka 30.

"Hilo suala la mabaraza ya ardhi linajulikana kuwa yanaharibu katika maeneo mengi, yanafanya kazi ya Mahakama kutoa haki ya ardhi, jambo ambalo ni kinyume na Katiba, nadhamiria kupeleka hoja binafsi katika Bunge lijalo, kupendekeza mabaraza haya kufutwa,” alisema Mchengerwa.

Sambamba na hilo, alisikiliza kero za wananchi ikiwa ni pamoja na migogoro ya ardhi kati ya wakulima na wafugaji, ambayo imekuwa  kilio kikubwa cha wananchi wa maeneo yote ya jimbo hilo, ambapo alisema anaijua changamoto hiyo na ameshaanza kuifanyia kazi kwa Baraza la Madiwani kuagiza mifugo ambayo ipo kinyume cha sheria kuondolewa ndani ya siku 30.

Hata hivyo, Mbunge huyo aliahidi kuchangia ujenzi wa zahanati, shule na barabara kwa kutoa mabati na saruji vyenye thamani ya Sh milioni 16.

"Nimesikia kero zenu za zahanati, shule na kufukia madimbwi barabarani; naanza na kuchangia mwenyewe saruji, mabati na fedha taslimu ili tuanze ujenzi, lakini nakuombeni nanyi mniunge mkono tujenge pamoja," alisema Mchengerwa.

Pia aliambiwa kero ya kukosekana kwa matuta barabarani, hali inayosababisha vifo vya watu kwa kugongwa na magari na pikipiki hali ambayo ilimfanya aoneshe mfano kwa kuweka matuta kadhaa kabla ya kuondoka mkutanoni hapo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo