Ufisadi NSSF usigeuzwe malumbano ya kisiasa


Mashaka Mgeta

Mashaka Mgeta
ZIPO tuhuma nyingi zinazotolewa nchini kuhusiana na matumizi mabaya madaraka, hujuma dhidi ya rasilimali za umma ama aina nyingine za ufisadi.

Kuibuliwa kwa tuhuma hizo na nyingine zinazofanana na hizo hakukuanza katika awamu ya tano chini ya Rais John Magufuli, la hasha.

Tuhuma kama hizo na nyinginezo zimekuwapo tangu wakati wa utawala wa awamu wa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Kambarage Nyerere na marais waliomfuata, Ali Hassan Mwinyi, Benjamin Mkapa na Jakaya Kikwete.

Kila Rais katika utawala wake, alizibaini tuhuma hizo na kuzishughulikia kwa namna yake, ile iliyotofautiana kutoka awamu moja hadi nyingine.

Lakini ukweli ni kwamba tuhuma za ufisadi zimekuwapo katika tawala zote na zikashughulikiwa kwa namna zinazotofautiana.

Hata sasa wakati Rais Magufuli akisadikiwa kuwa ‘mkali’ dhidi ya wanaohujumu rasilimali za umma ama kutumia vibaya madaraka yao, wapo waliobainika kuwa kinyume na mwelekeo huo, wakajiweka kando na azma njema ya kuondokana na uovu huo.

Ndio maana Rais Magufuli amejikuta mara kadhaa akilazimika kutengua uteuzi wa viongozi aliowakuta ama aliowateuwa, ili mradi tuhuma zinazotolewa dhidi yao hazikidhi vigezo na sifa za kiongozi anayepaswa kuutumikia umma katika utawala wake.

Hivi karibuni, kumeibuliwa kashfa inayolihusu Shirika la Taifa la Hifadhi ya Jamii (NSSF), kuhusu ununuzi wa ardhi ma ujenzi wa makazi katika eneo la Kigamboni jijini Dar es Salaam.

Zipo taarifa zinazodai kuwa NSSF ilinunua ekari 300 kwa kutoka kwa mbia mwenzake, kampuni ya Azimio Housing Estates (AHEL) kwa zaidi ya Sh milioni 800 kwa ekari.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, NSSF ikisaidikiwa kuwa miongoni mwa mashirika ya hifadhi yenye idadi kubwa ya wanachama, inamiliki viwanja vingine katika eneo hilo vikiwa na thamani ya Sh milioni 4.5 kwa ekari.

Lakini hata ujenzi wa makazi hayo kupitia mradi wa mji wa kisasa, unatajwa kughubikwa na ufisadi wa mabilioni ya Shilingi za kitanzania, hali inayoibua hoja za kuwapo uchunguzi wa kina na kuchukua hatua dhidi ya wahusika.

Ni jambo lililo wazi kwamba NSSF ni shirika la umma, raia wa Tanzania pasipo kujali itikadi, dini, kabila ama tofauti yoyote, ni wanachama kwa mujibu wa sheria zinazowaongoza.

Hivyo kuyumbishwa ama kuhujumiwa kwa NSSF kwa namna yoyote, maana yake ni kuyaathiri maslahi ya raia walio wengi, hivyo kuwa na athari kwa jamii pana ya Watanzania.

Sasa zinapotokea tuhuma, bila kujali ikiwa zimethibitishwa ama lah, zikaelekezwa kwa `shirika kubwa’ kama NSSF, hakuna sababu ya wenye dhamana za kisiasa, kuiondoa jamii kutoka kwenye hoja ya msingi na kujielekeza katika kukidhi matakwa binafsi ama ya chama cha siasa.

Kwa mfano, mwishoni mwa wiki iliyopita, kuliibuka majibizano ya haja yanayoendelea kujadiliwa na watu, kati ya Msemaji wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Christopher Ole Sendeka na chama cha ACT Wazalendo kinachoongozwa na Zitto Kabwe.

Asili ya majibizano hayo ni hoja ya Ole Sendeka kuhusu kumtilia shaka Zitto kwa kile anachokiita kuwa ni ‘kuishambulia’ Serikali ya Rais John Magufuli inayowajibika katika kuwashughulikia mafisadi.

Ole Sendeka akaenda mbele zaidi na kupendekeza Serikali kupitia vyombo mahususi, kuchunguza mali na akaunti za Zitto aliyekuwa kuwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC).

Hata hivyo, chama cha ACT Wazalendo kupitia kwa Habib Mchange, wakajibu hoja za Ole Sendeka, hivyo kuigeuza suala la msingi katika kuutafuta ukweli kuhusu ufisadi unaotajwa NSSF, kuwa la kisiasa.

Ninatambua uhuru wa kujieleza kwa kila raia, kwamba linapotokea jambo kama kashfa dhidi ya NSSF, wapo watakaojenga hoja tofauti, zile za kuuibua ukweli, kushawishi ama kujilinda dhidi ya tuhuma husika.

Lakini uhuru huo haupaswi kuwa wenye `kuiondoa mezani’ hoja mahususi ya vita dhidi ya ufisadi, ikafanywa kuwa malumbano na ‘mipasho’ ya kisiasa isiyokuwa na tija.

Tatizo la kijamii, linalotokea kwenye jamii na kuiathiri jamii husika, linapaswa kujadiliwa kwa msingi wa suala na si kumlenga mtu binafsi ama kutafuta kuungwa mkono ili kuiokoa hadhi ya chama cha siasa ama vinginevyo.

Jambo lililo wazi ni kwamba zipo tuhuma zinazoelekezwa kwa NSSF, kwamba katika utendaji kazi wake, imefikia wakati kukawapo mianya iliyotumika kufanya ufisadi unaoweza kuwaathiri wanachama na taifa kwa ujumla wake.

Tatizo la kijamii kama tuhuma dhidi ya ufisadi linapogeuzwa kuwa sehemu ya malumbano ya kisiasa, mwelekeo wa uliopo unabadilishwa kiasi kwamba hata wahusika wanaweza kuutumia mwanya huo kufanikisha nia ya kupotosha na kuuficha ukweli.

Kama wanasiasa wanakuwa sehemu ya jamii inayoguswa na uovu kama unaodaiwa kutokea NSSF, iweje waanze ‘kutupiana madongo’ badala ya kujielekeza katika suala linalohityaji ufumbuzi, nalo ni ufisadi?

Bahati nzuri Zitto na Ole Sendeka wamewahi kuwa wabunge, wakishiriki mijadala ikiwamo iliyowaunganisha wabunge pasipo kujali tofauti zao, wakautetea umma dhidi ya uovu.

Vivyo hivyo inapaswa kuwa hata sasa, wakati ambapo suala la msingi ni ufisadi unaodaiwa kufanyika NSSF, basi na iwe hivyo, kwamba kinachopaswa kufanyika ni kushughulikia ufisadi na si mashambulizi ya kisiasa dhidi ya mtu binafsi.
Mwisho
0754691540

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo