Mpango aipa NIC changamoto tano


Celina Mathew

Dk Philip Mpango
WAZIRI wa Fedha na Mipango, Dk Philip Mpango ameipa changamoto tano Bodi ya Shirika la Bima la Taifa (NIC), akiitaka kuhakikisha inapitia upya sheria, taratibu za kiutawala na masuala ya fedha, ili kuongeza ufanisi na weledi kiutendaji.

Akizungumza jijini hapa juzi wakati akizindua Bodi hiyo, Dk Mpango aliagiza ifanye kazi ili kwenda sambamba na kasi ya Serikali, ambayo ina mengi ya kufanya, ikiwamo kukusanya kwa uhakika mapato yake.

Alitaja mambo hayo kuwa ni kusambaza huduma za bima nchi nzima, kutoa elimu kwa wananchi kuhusu bima, ushindani katika soko huria, huduma za bima kwa wakulima, wafugaji na wavuvi pamoja na kujenga kada ya wataalamu wazalendo wa bima.

Katika maelezo yake, Dk Mpango alisema Bodi hiyo inapaswa kuwa na ubunifu na kusambaza huduma za bima nchi nzima, ili wananchi wenye kipato cha kati wanufaike nazo.

Aliitaka itoe elimu kwa wananchi kuhusu bima ya kisasa kwa kuwa wengi hawana uelewa kuhusu suala hilo na wanatarajia mifumo ya bima ya msingi tu jambo ambalo ni changamoto.

“Hata mimi kiongozi sina bima ya maisha na hata viongozi wengine pia hawana, unakuta mtu anamiliki nyumba na gari la thamani, lakini hana bima ya maisha hivyo ni vema elimu ya kutosha itolewe ili watu hai wajue maana na umuhimu wa matumizi yake,” alisema.

Aliongeza kuwa wizara yake imejipanga kuchukua hatua za kufuatilia taasisi zote zilizo chini ya Wizara ili kuhakikisha zinajiendesha kwa faida na nchi inafaidika na mapato yanayotokana na biashara wanazofanya.

Alisema anajua kuwa shirika lilipitia wakati mgumu miaka ya 90 kilipoundwa kikosi kazi cha shirika ili kuboresha huduma za bima.

“Angalieni masuala ya fedha, mikakati hata mazingira ya soko ambayo yanaweza kukwaza shirika ili mpate ufumbuzi wa matatizo yaliyo kwenye shirika hilo,” alisema.

Mwenyekiti wa Bodi hiyo, Laston Msongole alisema kuanzia mwezi ujao, NIC itagawanywa maeneo mawili; ya bima ya mali na bima ya ajali na taratibu zimekamilika.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo