Lusekelo: Nilihojiwa Polisi kwa hila


Waandishi Wetu

Anthony Lusekelo
MCHUNGAJI wa Kanisa la Maombezi (GRC) la Ubungo Kibangu, Anthony Lusekelo ametaja sababu za kukamatwa kwake na polisi, kisha kuhojiwa kwa saa kadhaa, akihusisha tukio hilo na mpango wa kutengenezwa unaofanywa na watu aliodai wamekuwa wakimfuatilia kwa takribani mwaka mmoja sasa.

Aidha, Lusekelo maarufu kwa jina la Mzee wa Upako, amesema hakumtukana mtu, bali alitumia maneno matatu yaliyomo kwenye Biblia; upumbuzu, ushenzi na ujinga kuelezea hoja zake na kisha kuyatafsiri maneno hayo.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na JAMBO LEO Lusekelo alisema si kila linalosemwa, lazima lijibiwe na kwamba kwa tukio hilo lililomkuta Jumanne iliyopita, kuna baadhi ya mambo yamekuzwa kuliko uhalisia.

“Hii ni kashfa?” alihoji Lusekelo na kuongeza: “Wale wanaofumaniwa na wake za watu kwenye nyumba za wageni wasemaje, wanaokutwa wakizini kwenye magari au kupigana na walevi nao wasemaje? Nilikuwa nyumbani kwangu kashfa iko wapi. Ni mambo ya kukuza haya sasa kosa langu liko wapi? Wanasema mimi mlevi, hivi wamenikuta nakunywa pombe wapi?”

Jumanne iliyopita mchungaji huyo alikamatwa na Polisi maeneo ya Kawe, wilayani Kinondoni, akidaiwa kufanya fujo kuanzia saa 11 alfajiri hadi saa tatu asubuhi alipochukuliwa na Polisi wa Kituo cha Kawe.

Taarifa za Mzee wa Upako kufanya vurugu zilisambaa katika mitandao mbalimbali ya kijamii, huku video aliyerekodiwa eneo la tukio, ikionesha gari ikiwa imepaki barabarani huku akilumbana na watu waliokuwa ndani ya nyumba na taarifa zaidi kueleza kuwa alikuwa amelewa chakari.

Taarifa hizo zinaeleza kuwa chanzo cha tukio hilo ni kulipiza kisasi kwa jirani zake wanaoishi katika moja ya nyumba zilizopo jirani na nyumba yake, ambao alidai wamekuwa wakimkebehi kuwa hafai kuwa mchungaji kwa sababu ya ulevi.

Baada ya purukushani hizo, majirani hao walipiga simu Polisi ambao walifika eneo hilo na kuondoka na mchungaji huyo.

Ijumaa iliyopita katika mkutano wake na wanahabari, Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro alisema Polisi inaendelea kufanya upelelezi dhidi ya tukio hilo.

Lakini juzi katika mahojiano na gazeti hili, Mchungaji Lusekelo alisema kuwa watu aliotofautiana nao si majirani zake, bali ni walinzi wa kampuni binafsi ya ulinzi aliodai kuwa kwa muda mrefu amekuwa akikutana nao wakitoka nyumbani kwake.

“Wakati naingia nyumbani kwangu nilikutana nao getini nikawauliza wametoka wapi? Badala ya kunijibu wakaanza kutoa lugha za matusi. Nilifanya hivyo kwa sababu ya usalama wangu na sikuwa nikifahamiana nao,” alisema.

Alisema baada ya kuanza kuwajibu walinzi hao, waliondoka eneo hilo na kuingia katika moja ya nyumba zilizopo katika mtaa anaoishi, “niliwafuata hapo getini na kuwaeleza kuwa sitoondoka mpaka Polisi waje ili kubaini ndani ya ile nyumba kuna nini.”

Alisema baada ya Polisi kufika eneo hilo hawakutaka kusikiliza  maelezo yake badala yake walimkamata.

“Wale sio majirani zangu…, hili jambo unaweza kulichukulia upendavyo ila binafsi naona kama ni tukio la kupanga kutokana na hali kama hii ya kukutana na watu nisiowafahamu kujitokeza mara kwa mara,” alisema.

Huku akionesha kushangazwa na jinsi habari hizo zilivyotikisa maeneo mbalimbali nchini, mchungaji Lusekelo alisema, “wakati mwingine unaweza kujiona mtu wa kawaida kumbe…, kwa kweli habari zile (kuhusu tukio hilo) ziliniogopesha sana, nadhani hata askari aliyenikamata anajuta kwa kutotaka kunisikiliza.”

“Wakati mwingine Mungu ana mambo yake, mambo yake yana siri nyingi. Kujibu sio busara sana,” alisema.

Mahubiri ya jana

Akiwahubiria  mamia ya waumini wake jana, Lusekelo alisema maneno upumbavu, ushenzi na ujinga siyo matusi,  bali ni maelezo kutoka ndani ya Biblia.

Akitafsiri maneno kwa mujibu wa kitabu hicho Lusekelo alisema neno mpumbavu maana yake ni mtu asiyefundishika kama wale wanawali sita ambao taa zao zilizimika kabla ya kuwasili kwa bwana harusi.

Kuhusu neno mshenzi, alisema maana yake ni mpagani asiye na hofu ya Mungu na mjinga ni mtu mwenye dhambi ya mauti anayestahili kutupwa jehanamu.

“Hayo ni maneno ambayo napenda kuyatumia kwa vile yapo kwenye Biblia na hata Yesu aliwahi kuyatumia, lakini nafahamu siyo vizuri kutoa lugha ya matusi,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo