Warioba: Uteuzi haunizibi midomo


Fidelis Butahe

Joseph Warioba
WAZIRI Mkuu mstaafu, Jaji Joseph Warioba, amesema kuteuliwa kwake na Rais John Magufuli kuwa Mkuu wa Chuo Kikuu cha Sokoine cha Kilimo (Sua) kusihusishwe na siasa wala msimamo wake,  ukiwamo wa mchakato wa Katiba Mpya.

Alisema alishangazwa na wanaohoji uteuzi huo bila kujiuliza umuhimu wa chuo hicho kwa Taifa wakati inafahamika kuwa Watanzania wengi wanaendesha maisha yao kwa kutegemea kilimo, ufugaji na uvuvi.

“Hivi watu wanaelewa maana ya mkuu wa chuo kweli? Hiki ni cheo cha heshima tu. Mtu anateuliwa aweze kusaidia mawazo. Hii si kazi ya kulipwa mshahara, hakuna kitu kama hicho,” alisema Jaji Warioba jana katika mahojiano na JAMBO LEO.

Alisema chuo hicho kinafundisha kilimo, ufugaji na uvuvi, shughuli ambazo kwa kiasi kikubwa ndio zinaendesha maisha ya Watanzania wengi.

“Nakwenda kusaidia ili chuo kitoe wataalamu wa kusaidia sekta muhimu nchini. Sipendi kuona kila jambo likihusishwa na Katiba, ina maana mimi sina mambo muhimu zaidi ya Katiba?” Alihoji.

Jaji Warioba ambaye pia ni Mwenyekiti wa Iliyokuwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba alitoa ufafanuzi huo baada ya kuulizwa na gazeti hili mikakati ya kusaidia chuo hicho na habari zinazoenezwa kupitia mitandaoni kuwa uteuzi huo utamfanya ashindwe kusimamia mambo anayoamini, likiwamo la Katiba inayotokana na maoni ya wananchi.

Baada ya Bunge Maalumu la Katiba kumaliza kazi yake ya kupitisha Katiba Inayopendekezwa huku baadhi ya maoni ya wananchi yakiondolewa, Jaji Warioba alikuwa miongoni mwa waliokosoa uamuzi huo, huku akihoji zaidi sababu za kuondolewa kwa miiko na maadili ya viongozi.

Mara ya mwisho kuzungumza na gazeti hili, Waziri Mkuu huyo wa zamani alisema atazungumzia mchakato wa Katiba-uliosimama mwaka jana-kupisha Uchaguzi Mkuu, baada ya Serikali kueleza hatua ambazo zitakazofuata.

Hata hivyo, Novemba 4 Rais Magufuli kwenye mkutano wake na wahariri wa vyombo vya habari alisema hakuna mahali alikoahidi kuendeleza mchakato wa Katiba Mpya.

Msimamo wake kuhusu Katiba ndio uliibua sintofahamu hiyo baada ya kuteuliwa na Rais Magufuli takribani siku tano zilizopita.

Alisema ni ajabu kuona baadhi ya wanahabari wakimhoji kuhusu msimamo wake na uteuzi huo badala ya kumwuliza atakisaidiaje chuo hicho.

Jaji Warioba ambaye alisisitiza kuzungumzia uteuzi huo kiundani baada ya taratibu kukamilika, alisema chuo kina umuhimu mkubwa kwa Taifa na kubainisha kuwa atahakikisha kinatoa wataalamu wa kutosha.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo