JPM asaini Sheria ya Habari


Fidelis Butahe

Dk. John Magufuli
AHADI ni deni. Ndivyo unavyoweza kusema baada ya Rais John Magufuli kutekeleza kwa kitendo kauli yake ya kusaini Muswada wa Sheria ya Huduma za Habari kuwa Sheria mara tu itakapotua mezani kwake.

Novemba 4 Rais alikutana na vyombo vya habari Ikulu, Dar es Salaam katika tukio ambalo liliwahusisha wahariri na kueleza kuwa Muswada wa sheria hiyo kama zilivyo zingine, zimefuata utaratibu wa kupelekwa bungeni na ukipitishwa na kuwa sheria atausaini haraka.

Jana Ikulu ilitoa taarifa ikieleza kuwa alisaini sheria hiyo juzi huku akipongeza wadau wote kwa kufanikisha kutungwa kwake.

“Kurugenzi ya Mawasiliano Ikulu inapewa kuwataarifu kuwa Rais amesaini Sheria ya Habari ya Mwaka 2016 iliyopitishwa na Bunge la 11 katika mkutano wake wa tano Dodoma,“ ilieleza taarifa ya Ikulu.

Katika taarifa hiyo, Rais Magufuli alisema, “naamini kuwa sheria hii itasaidia kuboresha sekta ya habari kwa manufaa ya wanataaluma wenyewe na Taifa.”

Uamuzi huo wa Rais Magufuli huenda ukawa mwiba mchungu kwa wadau wengi wa habari ambao walianza kupinga Muswada huo kuwasilishwa na kupitishwa na Bunge, wakitaka wapewe miezi mitatu ya kutoa maoni yao huku wakipendekezwa uwasilishwe bungeni mwakani.

Akizungumza hivi karibuni na JAMBO LEO Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria, Profesa Sifuni Mchome alisema sheria hiyo itaanza kutumika baada ya Waziri mwenye dhamana kuitangaza katika Gazeti la Serikali.

Alisema katika sehemu ya kwanza ya sheria hiyo, inaeleza kuwa itaanza kutumika baada ya kutangazwa kwenye Gazeti la Serikali, hivyo Rais akishaisaini ni lazima itangazwe kwanza ili ianze kutumika.

“Kama sheria husika imesema itatumika pale Waziri mwenye dhamana atakapoitangaza kwenye Gazeti la Serikali, basi utafuata utaratibu huo ila kwanza lazima iwe imesainiwa na Rais.

“Kama sheria husika haikusema, Waziri ataitangaza kwenye Gazeti la Serikali ili ianze kutumika, maana yake inaanza kutumika siku hiyo hiyo ambayo imesainiwa na Rais,” ilisema taarifa.

Kuhusu kanuni za sheria husika alisema haziwezi kusababisha sheria isianze kutumika, “Waziri husika anaweza kuziandaa kwa sababu kanuni ni suala endelevu…ila kama sheria inajitosheleza, itaanza kutumika kwa vipengee vyake kwa jinsi ilivyosema.”
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo