Waunga mkono marufuku ya majoho

Celina Mathew

BAADHI ya wabunge na wasomi wameunga mkono hatua ya Serikali kupiga marufuku matumizi ya majoho kwenye mahafali ya ngazi za chini za elimu na kueleza kuwa itarudisha nidhamu ya elimu.

Wakizungumza na JAMBO LEO kwa nyakati tofauti baadhi yao walisema suala hilo kwa kiasi kikubwa lilikuwa limefikia pabaya hali iliyosababisha vazi hilo kuonekana la kawaida tofauti na ilivyokuwa awali.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana alisema anaunga mkono hatua hiyo, kwa kuwa kila tasnia ina heshima zake na kwamba ni kama Jeshi hivyo si kila mtu anaweza kuvaa sare bila kigezo.

Alisema ipo haja ya kuheshimiwa kwa utamaduni, maana si kila mtu anavaa nyota, wala sare kama urembo bali lazima taratibu zifuatwe huku akihoji kuwa ni kwa nini suala hilo litokee nchini tu badala ya nchi nyingine.

“Hatuwezi kusema kila mtu atavaa gauni la harusi wakati si bibi harusi, hivyo wala haiwezekani vazi lile likavaliwa kwenye msiba au mahali pengine isipokuwa sehemu husika, ipo haja kwa vazi hilo lenye miiko na taratibu kuvaliwa linapotakiwa, maana kwa sasa unakuta hata mtoto wa chekechea au darasa la saba anavaa bila sababu za msingi,” alisema.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Juma Ngasongwa alisema joho ni kwa ajili ya watu waliosoma elimu fulani ya juu, kwa kuwa ni vazi la kuheshimika na si linavyotumika sasa hali inayosababisha kupoteza thamani yake.

Aliipongeza Serikali kwa hatua iliyofanya ili kuwe na kiwango cha kufanana watu wanapohitimu na kuvaa majoho hayo na si kama ilivyo sasa kila mtu anavaa bila sababu za msingi.

Mhadhiri wa UDSM, ambaye ni mtaalamu wa masuala ya lugha, Profesa Aldin Mutembei alisema Serikali imefanya vizuri kwa kuwa vazi hilo lilikuwa halivaliwi katika shule za msingi wala sekondari, bali ngazi za juu zenye sifa.

Alisema endapo vazi hilo litaendelea kuvaliwa kama ilivyo sasa, litaondoa tamaa ya watu kuendelea mbele kielimu, kwa kuwa linaonekana halina maana hadi mwanafunzi wa chekechea anavaa bila kujua maana yake.

Mbunge wa Ulyankulu, Joseph Kakunda alisema ili kuweka heshima inayostahili wanafunzi wavae joho wanapomaliza shahada zao kuanzia ya kwanza. Hiyo itasaidia kuwatia hamu walio katika ngazi za chini za elimu wajitahidi wafikie Chuo Kikuu.

Mbunge wa Songwe, Philipo Mlugo alisema anaunga mkono Serikali kusitisha uvaaji majoho kwa ngazi ya chini ya elimu kwa kuwa heshima ya wahitimu ilipotea kabisa.

“Zamani ukiona picha ya mtu kavaa joho na kofia yenye kamba unajua huyu kasoma hadi chuo kikuu, lakini leo huwezi kujua huyu aliyevaa joho ana shahada au kidato cha nne au ni stashahada.

“Sasa hivi hata chekechea wanavaa majoho. Nadhani kuanzia mwakani wahitimu wa ngazi mbalimbali wasiruhusiwe kuvaa majoho zaidi ya wanachuo wanaomaliza shahada zao na kuendelea”.

Mbunge wa Igalula, Musa Ntimizi alisema elimu ya chuo kikuu kupata shahada ni heshima kubwa zaidi katika ngazi hizo ni vema ikaheshimiwa na kuonesha upekee.

“Tunaheshimu ngazi nyingine za elimu za chini ila hii ni ya heshima zaidi tusiiache isifananishwe na za chini, mtoto asione tofauti ya kidato cha nne na chuo kikuu, joho liachwe chuo kikuu lioneshe heshima utofauti,” alisema.

Mwishoni mwa wiki, Waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Ufundi, Profesa Joyce Ndalichako, alipiga marufuku matumizi ya majoho kwenye sherehe za mahafali ya ngazi za chini za elimu na kutaka litumike kuanzia ngazi ya Shahada ili kulipa heshima vazi hilo.

Waziri Ndalichako alitoa kauli hiyo Mbeya wakati alipokuwa anawatunuku vyeti wahitimu wa mafunzo ya uongozi na usimamizi wa elimu kwa njia ya masafa, iliyotolewa na Wakala wa Usimamizi na Uongozi wa Elimu Nchini (Adem).
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo