Mbunge kupambana na changamoto jimboni


Joseph Sabinus

Janeth Mbene
MBUNGE wa Ileje, Janet Mbene (CCM) ameahidi kuhakikisha changamoto kuu za jimbo hilo za elimu, afya na barabara zinapata ufumbuzi wa kudumu.

Mbene alisema hayo hivi karibuni wakati akipokea msaada wa vitabu vya Sayansi na Hisabati vyenye thamani ya takribani Sh milioni tano kutoka ubalozi wa China nchini kwa ajili ya sekondari za jimbo hilo.

Katika hafla hiyo iliyofanyika kwenye ubalozi huo Dar es Salaam, Mbunge huyo alisema upungufu wa vitabu katika shule jimboni mwake, ni moja ya changamoto zinazotokana na maendeleo katika sekta ya elimu.

“Maendeleo mengine husababisha changamoto, mfano tangu Serikali ianze kutoa elimu bure hadi sekondari, kumekuwa na mwamko mkubwa wa wanafunzi.

“Changamoto zilizojitokeza kwa mafanikio hayo, ni uhaba wa vitabu, vifaa vya kufundishia, miundombinu ya vyumba vya madarasa na ukosefu wa mabweni hasa ya wasichana sekondari,” alisema Mbene.

Alisema ukosefu wa mabweni katika sekondari, ni tishio kwa maendeleo ya elimu kwa watoto wa kike kwa kuwa unachangia utoro, mimba na wasichana kutofanya vizuri kwenye masomo kwa kukosa muda wa kutosha kufuatilia masomo.

“Nashukuru ubalozi wa China kwa kuitikia ombi hili. Tutahakikisha vitabu hivi vinatumika vizuri ili shule zote zinufaike maana ni wajibu wangu kutafuta namna ya kutatua kero za wananchi wangu likiwamo suala la elimu, barabara na huduma za afya; hayo ni mambo makubwa yanayoninyima usingizi.

“Katika Jimbo hili, hakuna sekondari yenye bweni la wasichana. Nataka kuhakikisha hilo linaondoka na hii itasaidia kuwa moja ya dawa dhidi ya mimba za utotoni kwa wanafunzi,” alisema.

Akikabidhi msaada huo kwa niaba ya Balozi wa China, Ofisa Ubalozi huo, Gov Haodong alisema China inapata faraja kushirikiana na Tanzania kutatua kero za watoto katika sekta ya elimu.

“China itaendelea kushirikiana na Tanzania kuchangia elimu nchini maana China kuna usemi kuwa, “watoto na wanafunzi ndio maua ya Taifa”.

“Ingawa msaada huo ni mdogo, lakini kitu kidogo kinapotolewa kwa nia njema, kinakuwa na thamani kubwa, hivyo tutaendelea kukuunga mkono ili kusaidia watoto wetu,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo