Afya yalipa 300,000 deni NHC


Fidelis Butahe

SIKU chache baada ya Rais John Magufuli kuagiza Shirika la Nyumba la Taifa (NHC), lizitimue wizara na taasisi zote zinazodaiwa mamilioni ya kodi ya pango, kauli hiyo imezitetemesha wizara hizo ambazo sasa zimelipa malimbikizo yanayofikia Sh. bilioni 8.

Jana NHC ilitangaza kupokea fedha hizo zilizolipwa na taasisi za Serikali na watu binafsi,  likieleza zimeelekezwa katika ujenzi wa nyumba 300 za makazi mkoani Dodoma.

Malipo hayo yamefanyika baada ya agizo la Rais John Magufuli alilolitoa Septemba 7 mwaka huu, kwa kuzitaka wizara zote zinazodaiwa na shirika hilo kuwa zimelipa madeni hayo na zikishindwa ziondolewe kama ilivyokuwa kwa kampuni ya Mbowe Hotels inayomilikiwa na mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe.

Katika orodha ya taasisi zilizolipa, Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Ofisi ya Makamu wa Rais-Muungano na Mazingira na Wizara ya Elimu ndio zimemaliza deni lote, huku Wizara ya Afya ikilipa Sh 300,000 tu katika deni la Sh bilioni 1.4.

Akizungumza na waandishi wa habari jana Mkurugenzi wa Utawala wa shirika hilo, Raymond Mndolwa, alisema taasisi za Serikali zilikuwa zikidaiwa Sh bilioni 9.3 na watu binafsi Sh bilioni 4.

“Kulipwa kwa madeni haya ni miujiza kwa kweli tunamshukuru Rais Magufuli. Sh bilioni 5.9 zimeshalipwa na taasisi za Serikali zilizokuwa zikidaiwa na sasa deni limebaki Sh bilioni 3.3,” alisema

Alisema malipo hayo ni sehemu kidogo ya idara na taasisi za serikali zilizopanga katika majengo ya shirika hilo na kubainisha kuwa wameamua kupeleka kiasi hicho cha fedha katika ujenzi wa nyumba eneo la Iyumbu, Dodoma kuunga mkono mpango wa Serikali kuhamia Dodoma.

“Ujenzi wa nyumba hizi tayari umeshaanza. Kuna taasisi hazijalipa deni lote ila tumeingia makubaliano maalumu. Kama walikuwa na deni la nyuma wataendelea kulilipa ila lile deni la kila mwezi ni lazima lilipwe,” alisema Mndolwa.

“Tunaendelea kufuatilia deni ili na tunaamini idara na taasisi husika zitamaliza deni ifikapo mwisho wa mwezi Desemba.”

Kuhusu watu binafsi, Mndolwa alisema licha ya baadhi kulipa, wapo ambao wanaendelea kulimbikiza madeni yao huku akibainisha kuwa hivi karibuni watafanza zoezi kabambe la kuwaondoa wadaiwa wote.

“Tutawaondoa katika majengo ya shirika na kuuza samani kufidia deni wanalodaiwa, kuwatoa katika vyombo vya habari na kuwapeleka mahakamani ili walipe deni,” alisema.

Alisema kati ya Sh bilioni 4 waliozokuwa wakidaiwa watu binafsi, wamelipa Sh bilioni 2 tu na kwamba katika wilaya ya Ilala wameondoa watu 40 katika majengo ya shirika hilo, zoezi ambalo litafanyika Upanga, Temeke na Kinondoni.

“Kwa watu binafsi mazungumzo hakuna. Haiwezekani tukudai Sh360,000 kwa mwezi na ushindwe kulipa mwaka mzima huku ukiwa kimya. Tukikukuta tunakutoa nje,” alisisitiza.

Katika orodha ya wadaiwa hao, Wizara ya Habari, licha ya kulipa Sh milioni 70, bado inadaiwa Sh bilioni 1.1, huku Wizara ya Ujenzi  ikilipa Sh bilioni 2.1 na kubakisha deni la Sh milioni 58.
Ends  

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo