Watendaji Wizara ya Afya lawamani


Badrudin Yahaya na Charles James

Ummy Mwalimu
BAADHI ya watumishi wa Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, wametupiwa lawama kwa kushindwa kutimiza wajibu wao kwa jamii na kukwamisha taasisi binafsi kushindwa kufungua hospitali za kisasa nchini.

Kampuni ya Quality Health Limited ya jijini Dar es Salaam ambayo ina mpango wa kufungua kliniki na maabara zaidi ya 4,000 nchini ni miongoni mwa taasisi binafsi zilizokwamishwa na watendaji hao wa wizara.

JAMBO LEO, limeona baadhi ya maombi ya Quality Health Limited kwenda Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto yakiwa na mchanganuo wa namna kliniki hizo zitakavyofanya kazi kwa ajili ya kuwahudumia Watanzania.

“Quality Health Limited imekusudia kufungua kliniki na maabara za kisasa zaidi ya 4,000 nchi nzima ambazo zitakuwa zikitoa huduma ya afya kwa gharama nafuu kwa kusaidiana na Serikali katika kuwapatia huduma bora wananchi hususan wagonjwa.

“Lakini jambo la kusikitisha ni kwamba tunakutana na vikwazo vingi ambavyo vinakatisha tamaa. Tunatambua kuwa kuna maeneo mengi tu nchini yanakabiliwa na ukosefu wa huduma ya afya, hivyo sisi tunataka kuondoa hali hiyo kwa kusaidiana na serikali yetu,” alisema ofisa mmoja wa kampuni hiyo.

Ofisa huyo alisema katika mchakato wa kufungua huduma hiyo ya afya wameshatumia zaidi ya sh. milioni 90, hivyo wanashangaa kuona wakikwamishwa kwenye hatua za mwisho.

Alisema kuwa Serikali ya Awamu ya Tano ina nia thabiti ya kuwapatia wananchi wake huduma bora ikiwemo ya afya na kwamba hata, Waziri Ummy Mwalimu amekuwa akifanya kazi kubwa lakini wapo baadhi ya watendaji wanarudisha maendeleo nyuma.

Alifafanua kuwa ana mpango wa kufungua vituo vingi zaidi vya afya ambavyo vingekuwa na uhusiano wa karibu na madaktari bingwa kutoka katika maeneo mbalimbali na kwamba hiyo ingechangia kuinua sekta ya afya hasa kwa wananchi wa hali ya chini.

Historia ya Tanzania inaonesha zaidi ya robo tatu ya wananchi wamezaliwa na kukulia katika maeneo ya vijijini sehemu ambazo hazina huduma bora ya afya, hivyo endapo wawekezaji binafsi wakiruhusiwa kuwekeza ni wazi itasaidia kuinua sekta hiyo na kutoa nafuu kwa hospitali za serikali kuelemewa na wingi wa wagonjwa.

Alidai kuwa Halmashauri ya Wilaya ya Temeke na Mamlaka ya Usalama na Afya Mahali pa Kazi (OSHA) iliwaruhusu kufungua kliniki katika Jengo la Quality Centre jijini humo, lakini wakakutana na vikwazo kutoka kwa maofisa wa wizara kwamba eneo hilo halitakiwi kuwa na kliniki.

Aliiomba Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) kuingilia kati suala hilo na kuona kama michakato yake ina uhalali kwani kuna baadhi ya kliniki zimeanzishwa wakati hazijatimiza vigezo.

Ofisa huyo kutoka Quality Health Limited, alisema vikwazo wanavyokutana navyo vinawakatisha tamaa na vinawanyima fursa mamilioni ya Watanzania ambao walistahili kupata huduma bora ya afya kwa gharama nafuu.

“Inakatisha tamaa kwa kweli hebu jaribu kufikiria mtu unataka kufungua hospitali ambazo zitasaidia Watanzania wote, lakini unanyimwa kibali, na kinachohuzunisha zaidi haupewi sababu za msingi bali unapigwa danadana nyingi zisizo na msingi wowote,” alidai.

JAMBO LEO lilipomtafuta Msajili wa Hospitali kutoka wizarani, Dk Pamela Sawa alisema hawezi kuwazungumzia wawekezaji hao, kwani hakuna watu waliokuja ofisini kwake wakanyimwa usajili wa kutoa huduma ya afya.

Dk Sawa alisema ili mtu aweze kupatiwa usajili lazima kwanza asajili jina la kampuni yake kisha aende ofisini kwake, ambapo atapatiwa vigezo ambavyo vinahitajika na kama atakuwa navyo wizara haitasita kuwapatia usajili.

“Hakuna wawekezaji waliotaka kupatiwa usajili wa kufungua vituo vya afya wakanyimwa na ofisi yangu, labda kama hawakua na vigezo tunavyovihitaji, lakini kama wamekidhi niwahakikishie wizara inatoa kibali kwa kila mtu mwenye sifa na kama wanasumbuliwa na watendaji wengine basi waonane na mimi moja kwa moja,” alisema Dk Sawa.

Alisema wizara na ofisi yake vinafanya kazi na watu wa aina zote bila kubagua na endapo kuna wawekezaji wenye vigezo wanaohitaji usajili anawakaribisha ofisini kwake waweze kufanya kazi.



Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo