Shule yafungwa bila kufanya mitihani


Warioba Igombe, Morogoro

WANAFUNZI wa sekondari ya Mtoni Moro mkoani hapa, wamefunga shule bila kufanya mitihani ya muhula huku Mkuu wa Shule akituhumiwa kwa ubadhirifu wa fedha za ada.

Kwa mujibu wa mtoa taarifa ambaye hakutaka jina lake litajwe,     urasimu wa Mkuu wa Shule, Mhina Mlimbo umesababisha shule kufungwa mapema tofauti na shule zingine nchini.

Alidai kuwa shule hiyo ilifungwa Oktoba 15 badala ya Novemba, huku wanafunzi wakiwa hawajafanya mtihani kama ilivyo kawaida ya shule zote nchini kufanya mitihani ya muhula kabla ya shule kufungwa.

“Kuna mambo mengi sana hapa shule yanayokera walimu na wazazi kutokana na vitendo vinavyofanywa na Mkuu wa Shule, kitendo kilichosababisha wanafunzi kufunga shule mapema tofauti na shule zingine,” alisema mtoa taarifa.

Alisema mbali na ubadhirifu uliosababisha walimu kutolipwa mishahara yao tangu Januari, shule hiyo pia haina Bodi, Bendera ya Taifa, wala picha ya Rais.

Alisema iwapo hatua kali hazitachukuliwa dhidi ya wahusika, wanafunzi wanaosoma shule hiyo watafeli masomo yao pamoja na mitihani ya Taifa akidai kuwa Mkuu wa Shule anajali maslahi yake pekee.

Hata hivyo, Mlimbo alikanusha tuhuma hizo akisema ni za uongo na kueleza kuwa zinaenezwa na mmoja wa walimu ambaye alifukuzwa kazi shuleni hapo baada ya kutaka kumsaidia mwanafunzi mtihani wa Taifa.

Kuhusu kufunga shule mapema, Mlimbo alisema shule yake ilifungwa mapema ili kupisha mitihani ya Taifa ya kidato cha nne, ili wanafunzi waweze kufanya mitihani katika hali ya utulivu bila bughudha.

Mkurugenzi wa Shule hiyo, Bernadeta Masuka alikiri kupokea tuhuma hizo akiisema kwa sasa hawezi kutoa tamko lolote, kwani afya yake si nzuri na itakapoimarika atashughulikia changamoto zote za shule hiyo.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo