Atakayetoa lugha ya matusi kwa wajawazito kukiona


Sijawa Omary, Mtwara

Ummy Mwalimu
SERIKALI imewataka watumishi wa sekta ya afya wenye tabia ya kuwatolea lugha ya matusi kina mama wajawazito wanaoenda kupata huduma ya kujifungua kuacha mara moja vinginevyo imejipanga kuwashughulikia.

Wito huo umetolewa juzi na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Wazee na Watoto, Ummy Mwalimu alipokuwa akizungumza na wananchi mkoani Mtwara katika Viwanja vya Mashujaa kwenye Uzinduzi wa Mradi wa Tumaini la Mama (KFW) katika mikoa ya Mtwara na Lindi.

Wito huo umekuja, baada ya kinamama hao kutoa malalamiko hayo mbele ya waziri Ummy kuhusu baadhi ya watumishi wa afya kwa kinachodaiwa wamekuwa wakitoa lugha ya matusi kwa wagonjwa.

“Marufuku kutoa lugha ya matusi kwa akina mama wanapokuja kujifungua na yoyote atakayeripotiwa kwa kutajwa jina nasema hivi nitaimba na wewe. Kwa hiyo kina mama niwaombe ukimfahamu huyo mtumishi anayekutolea lugha ya matusi tunaomba utupatie jina lake,” alisema Ummy.

Katika hatua nyingine, Benki ya Maendeleo ya Ujerumani (Kfw) kwa kushirikiana na Serikali imeandaa mkakati wa kuwasaidia kinamama na watoto lengo likiwa kupunguza vifo wakati wa kujifungua na vya watoto hao chini ya miaka mitato.

Taarifa zinaonesha kwamba hadi mwaka 2015, watoto 54 kati ya 1,000 hufariki dunia kabla ya kufikisha miaka mitano.

Hatua hiyo imefikiwa ikilinganishwa na idadi ya mwaka 2005 ambapo watoto zaidi ya 112 kati ya kila watoto 1000 walifariki dunia.

Mwakilishi wa ubalozi wa  Ujerumani nchini, Julia Hanninga ambao ndiyo watekelezaji wa mradi huo alisema mradi huo katika mikoa hiyo ya Mtwara na Lindi unatekelezwa kwa awamu ya pili.

Mradi huo hadi hivi sasa tayari umeshatekelezwa katika maeneo matano, ikiwemo mkoa wa Mbeya, Tanga, Songwe na mikoa hiyo ya Mtwara na Lindi.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo