Sheria kurekebishwa kubana mafisadi


Wankyo Gati, Arusha

SERIKALI imeanza kurekebisha sheria ya kuzuia na kupambana na rushwa ili kubana zaidi mafisadi na kuzuia mianya ya ulaji rushwa.

Hayo yalibainishwa jana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Anjela Kairuki kwenye mkutano wa kujadili masuala ya kiuchunguzi wa mali ambazo zinapatikana kwa njia ya rushwa.

Na pia kuchunguza na kubaini mali zilizofichwa katika nchi zingine, ulioshirikisha nchi nane za Mashariki mwa Afrika zenye taasisi za kuzuia na kupambana na rushwa.

Alisema Serikali imeanza mchakato wa kurekebisha sheria hiyo na inasubiri Bunge lijalo kuwasilisha bungeni Muswada wa Marekebisho ili ujadiliwe na kupitishwa.

Alisema sheria iliyopo sasa haibani mafisadi wala wala rushwa na  wapokea rushwa, kwani faini ambazo wanapigwa watuhumiwa hawa ni ndogo kuliko kosa alilotenda.

"Unakuta adhabu zinazotolewa haziendani kabisa na hasara inayosababishwa na mkosaji, unakuta mkosaji anasababisha hasara ya mabilioni ya fedha, lakini analipwa fedha kidogo tu, hivyo ndio maana tumeona tufanyie marekebisho sheria hii ili kuwabana zaidi," alisema Kairuki.

Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Valentino Mlowola alisema kwa kipindi hiki kumekuwa na ongezeko la wananchi ambao wanatoa taarifa za watoa rushwa, waomba rushwa na mafisadi hii inaonesha jinsi gani wananchi hawa wameelimika na wameelewa athari za rushwa.

Alisema hadi mwezi jana Takukuru ilikuwa imekusanya Sh bilioni 45, sawa na asilimia 500 za fedha zilizokuwa zimefichwa nchi zingine na ambazo zilikutwa kwa mafisadi na kutolewa kutokana na watuhumiwa watoa na wapokea rushwa.

"Aidha, napenda kutoa mwito kwa wananchi kuendelea kutoa taarifa za watu ambao wamejipatia fedha haramu, wenye mali zilizotokana na rushwa na wanapotoa taarifa wasiwe waoga, kwani kuna sheria inayowalinda na wanapotakiwa kutoa ushahidi wasiogope kwani sharia pia inamlinda mtoa taarifa,” alisema Mlowola.

Mkurugenzi Mtendaji wa Sekta Binafsi Tanzania, Godfrey Simbeye alimpongeza Rais John Magufuli kwa kuanzisha Mahakama ya Mafisadi, kwani ni jambo ambalo walikuwa wakilitamani kwa muda mrefu.

Alisema wao wako tayari kushirikiana na Serikali kukomesha  tatizo la rushwa na wanaojipatia fedha na mali kwa njia ya rushwa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo