NMB yaipa Serikali kompyuta 250


Moi Dodo

BENKI ya NMB imetoa kompyuta 250 kwa Serikali zilizounganishwa na mkongo wa Taifa, ambazo zitatumika kufundishia Tehama na masomo mengine kwa shule za msingi na sekondari.

Akizungumza wakati wa hafla ya makabidhiano ya kompyuta hizo juzi, Katibu Mkuu wa Wizara ya Ujenzi, Mawasiliano na Uchukuzi, Profesa Faustin Kamuzora alisema msaada huo utainua elimu nchini.

Profesa Kamuzora ambaye alipokea kompyuta hizo kwa niaba ya Waziri wa Ujenzi, Mwasiliano na Uchukuzi, Profesa Makame Mabarawa alisema msaada huo umekuja wakati mwafaka, kwani Taifa linahitaji wataalamu wa kompyuta ambao watasaidia kuunda programu muhimu kwa sekta ya elimu na Taifa kwa ujumla.

“Maendeleo ya teknolojia yanazidi kukua na ili kuendana nayo ni vema tukaanza kumfundisha mtoto elimu ya kompyuta akiwa mdogo au kwenye ngazi za chini.

“Hivyo msaada wenu NMB utaharakisha ufundishaji wa Tehama katika shule za msingi na sekondari. Vijana wanatakiwa wafundishwe mapema elimu hiyo ili wapate kuunda programu mahususi kwa Taifa.

“Kila taifa linajivunia wataalamu wake, hivyo msaada huu naamini utakuwa chachu ya upatikanaji wa wataalamu hao,” alisema Profesa Kamuzora.

Mkurugenzi Mtendaji wa NMB, Ineke Bussemaker alisema benki hiyo imetoa msaada huo ikiamini utakuwa mwanzo wa maendeleo ya elimu ya kompyuta nchini kwa wanafunzi wa msingi na sekondari.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo