Rais wa Zambia kuzuru nchini keshokutwa


Abraham Ntambara

Rais Edgar Lungu
RAIS wa Zambia, Edgar Lungu, anatarajiwa kuwasili nchini keshokutwa kwa ziara ya siku tatu ambapo pamoja na mambo mengine, atatembelea Reli ya Tazara na Bomba la Mafuta (Tazama).

Katika ziara hiyo ya kiserikali, Zambia na Tanzania zinatarajiwa kusaini mikataba minne ya ushirikiano ya kuboresha namna bora ya ufanyaji kazi wa Tazara na Tazama.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki na Kikanda, Dk Augustine Mahiga aliwaambia waandishi wa habari jana Dar es Salaam, kwamba Rais Lungu anatarajiwa kuanza ziara hiyo Novemba 27 na atakuwa nchini hadi Novemba 29.

“Rais John Magufuli, ametoa mwaliko kwa Rais Edgar Lungu wa Zambia na tunatarajia kuupokea ugeni huo Novemba 27, Jumapili hii. Atatembelea vituo vikuu viwili vinavyotuunganisha, Tazara na Tazama,” alisema Dk Mahiga.

Alisema madhumuni ya ujenzi wa Reli ya Tazara yalikuwa ni kwa ajili ya maendeleo ya kiuchumi ya nchi hizo mbili pia kusaidia ukombozi kwa nchi za Kusini mwa Afrika na ndiyo sababu ilijulikana kama Reli ya Uhuru.

Aidha, aliongeza kuwa kwa upande wa bomba la mafuta lilijengwa ili kuirahisishia Zambia kusafirisha mafuta kutokana na ugumu uliokuwepo baada ya kuwekewa vikwazo na Afrika Kusini.

“Kutokana na vikwazo ambavyo Zambia iliwekewa na Afrika Kusini, Mwalimu Julius Nyerere na Dk Kenneth Kaunda wakajenga hili bomba ili kuepuka vikwazo,” alisema Dk Mahiga.

Alisema pia Rais Lungu atatembelea kisima cha kuhifadhi mafuta ghafi na kwamba anaamini ujio wake utasaidia kutatua changamoto zinazokabili Tazara na Tazama.

Waziri Mahiga alisema kabla ya kumaliza ziara, Rais Lungu atatembelea bandari ya Dar es Salaam kuangalia sehemu ambako mizigo ya Zambia huhifadhiwa kabala ya kusafirishwa kwa barabara.

Balozi wa Tanzania nchini Zambia, Grace Mujama alisema matarajio ya Zambia ni kwamba baada ya changamoto za bandari ya Dar es Salaam na Reli ya Tazara kutatuliwa, wafanyabiashara watarudi, kwani waliihama bandari ili kutafuta urahisi wa usafirishaji mizigo.

“Wazambia walihama Bandari ili kutafuta urahisi wa usafiri, inabidi kuangalia namna ya kuboresha ili warudi,” alisema Grace.

Balozi Samwel Shelukindo ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Afrika, Wizara ya Mambo ya Nje, alisema mbali na mikataba hiyo minne itakayosainiwa wataweka utaratibu wa ushirikiano katika sekta ya Uhamiaji, Magereza na Ushirikano kwenye usafiri wa anga.

“Tutasaini makubaliano pia ya ushirikiano katika sekta ya Uhamiaji na Magereza, kwa mfano kuna Watanzania waliofungwa Zambia na pia Wazambia wapo hapa, pia tutakubaliana juu ya ushirikiano kwenye usafiri wa anga,” alisema Shelukindo.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo