Wasomi wampongeza JPM kwa uhakiki wa vyeti


Francis Godwin, Iringa

Rais John Magufuli
UONGOZI  wa  Chuo Kikuu cha Iringa (UoI) umempongeza  Rais John Magufuli na Serikali yake ya Awamu ya Tano kwa  jitihada  anazozifanywa katika uhakiki wa   watumishi  hewa na wenye  vyeti  bandia, kikieleza  kuwa hatua   hiyo  ni  nzuri na  itasaidia kupata  wataalamu wenye  sifa.

Mwenyekiti wa Bodi ya UoI, Askofu Dk. Odenburg  Mdegela wa Kanisa la Kiinjili  la Kilutheri Tanzania (KKKT) Dayosisi ya  Iringa,  alitoa pondezi hizo akisema zoezi hilo linapembua mchele na chuya na kuwaacha wenye vyeti halali pekee.

“Si sahihi mtu mmoja akae darasani miaka mitatu na mwingine apate cheti kutoka Kariakoo tena kikiwa na ufaulu wa juu kuliko yule aliyekaa darasani,” alisema Askofu Mdegela.

Alisema watu hao wanapokutana kazini yule aliyepata vyeti bandia vyenye ufaulu wa juu anakuwa hajui kazi jambo lililokuwa likirudisha nyuma maendeleo ya taasisi nyingi na Taifa kwa jumla.

“Uhakiki wa vyeti unapaswa kuungwa mkono na wadau wote wakiwemo wa elimu kwa kuwa hali ilikuwa mbaya, huku wale wenye vyeti bandia vikiwa na ufaulu wa hali ya juu ilhali hawajui kazi,” alisema Mdegela

Alisema chuo hicho kinajipanga kuachana na mtazamo uliojengeka kwa muda mrefu wa kujiendesha kwa kutegemea wafadhili mbalimbali wa ndani na nje ya nchi pamoja na mikopo ya ada za wanafunzi kutoka serikalini.

Alisema wanatarajia kuanzisha asasi itakayokuwa imeunganishwa na chuo itakayotoa mikopo kwa ajili ya wanafunzi wanaokwama kupata huduma hiyo kutoka maeneo mengine.

Mkuu wa chuo hicho, Jaji Mkuu mstaafu Augustine Ramadhani alisema ni vema wahitimu wakawa wazalendo kwa nchi yao na kuitumia elimu waliyoipata kwa maendeleo ya watanzania wote.

Makamu Mkuu wa UoI, Profesa Joseph Madumula alisema mazingira ya utoaji wa elimu kwa sasa yamekuwa na ushindani mkubwa tofauti na miaka ya nyuma ambapo kulikuwa na chuo kikuu kimoja cha Dar es Salaam kikiwa na matawi mawili ya Sokoine na Muhimbili.

Aliongeza kuwa kwa sasa kuna zaidi ya vyuo vikuu 60 vya binafsi na serikali lakini idadi ya wanafunzi wanaodahiliwa haijaongezeka kulingana na vyuo idadi ya vyuo.

Alisema wamejipanga kutoa elimu shirikishi ya ujasiliamali kwa wanafunzi wote wa Chuo hicho ili wakimaliza wasitegemee kuajiriwa tu bali wawe na uwezo wa kujiajiri na kuzalisha ajira kwa vijana wengine.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo