Mchungaji Lusekelo aingia matatani


Fidelis Butahe

Anthony Lusekelo
MCHUNGAJI wa Kanisa la Maombezi (GRC) la Ubungo Kibangu, Anthony Lusekelo, ameingia matatani baada ya kudaiwa kuwatolea lugha chafu majirani zake na kuanzisha vurugu akipinga kuitwa mlevi, jambo lililosababisha ashikiliwe kwa saa kadhaa na Polisi baada ya kukamatwa.

Tukio hilo la aina yake ambalo Kamanda wa Polisi Kanda Maalumu ya Dar es Salaam, Simon Sirro ameiambia JAMBO LEO kuwa atalitolea ufafanuzi leo katika mkutano wake na wanahabari, lilitokea juzi asubuhi baada ya Mchungaji huyo kupishana kauli na majirani hao karibu na nyumba anamoishi iliyopo Kawe, Dar es Salaam.

Lusekelo jana alilitaka gazeti hili kupuuza habari hizo kwa maelezo kuwa ni za uzushi na hata alipoelezwa kuwa amerekodiwa, akionekana anatoa lugha chafu kwa majirani hao na kutishia kuwaua, alisisitiza zipuuzwe.

“Achana nao hao ni uzushi tu huo, hao watakaoandika shauri yao. Kila jambo ukijibu si sahihi, wao wameona hivyo na kutafsiri hivyo shauri yao,” alisema Mchungaji Lusekelo.

Baadhi ya mashuhuda wa tukio hilo walitumia simu zao za mkononi na kumrekodi Mchungaji huyo, wakati akiporomosha matusi hayo, kuonekana akitoa vitisho na kugoma kuliondoa gari lake alilokuwa ameegesha kwenye mtaa anaoishi, hali iliyosababisha magari mengine kushindwa kupita.

Katika taarifa hizo na baadhi ya picha hizo za video, zinamwonesha Mchungaji huyo akiombwa na watu wanaomfahamu kuacha kutoa lugha chafu hadharani, kwa kuwa ni kiongozi wa kiroho, lakini alipinga kwa maelezo kuwa majirani hao wanamdhihaki muda mrefu kwa kumwita mlevi.

Taarifa zaidi zinaeleza kuwa Mchungaji huyo aliyedaiwa kuwa alikuwa amezidiwa na kilevi:

“Tulimsihi aingie ndani mwake…vijana wake walifungua lango na akaingia ndani na kusema ndio alikuwa anarudi tangu alivyoondoa Jumanne wiki hii… Licha ya kumsihi asitoke tena nje, lakini aliongozana na vijana hao hadi nje na kuendelea kutukana majirani hao huku akinyeshewa mvua na alikuwa hajavaa viatu,” zilieleza habari hizo.

Baada ya Mchungaji huyo kuonekana kutokuwa tayari kutulia, baadhi ya majirani walipiga simu Polisi, ambao walifika eneo hilo na kumkamata.

Akizungumza tukio hilo, Kamanda Sirro alisema atalitolea ufafanuzi leo. Awali gazeti hili lilizungumza na Kamanda wa Polisi Kinondoni, Susan Kaganda aligoma kusema lolote, akitaka atafutwe Kamanda huyo wa Kanda Maalumu.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo