Wazazi watelekeza mtoto mochari mwezi


Mwandishi Wetu

MWILI wa mtoto Justine Chedega (6) aliyefariki dunia akipatiwa matibabu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili (MNH), Kitengo Cha Mifupa (MOI) umetelekezwa mochari na familia yake kwa takribani siku 24.

Taarifa ambazo JAMBO LEO, ilizipata jana kutoka Moi, zilisema mtoto huyo alifariki dunia Oktoba 28 wakati akitibiwa baada ya kupata ajali ya kugongwa na pikipiki.

“Mtoto huyo alifikishwa hapa Oktoba 23 na kufariki dunia Oktoba 28, hadi leo mwili wake uko mochari, ndugu zake hawaonekani,” kilisema chanzo hicho.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Justine alifikishwa hospitalini hapo akitokea hospitali ya Temeke alikofikishwa awali baada ya ajali.

Chanzo cha kutelekezwa kwa mwili wa mtoto huyo kinatajwa kuwa utata wa jina aliloandikishwa baada ya kufikishwa hospitalini.

Kwa mujibu wa taarifa za kiuchunguzi ndani ya hospitalini hiyo, Justine alifikishwa MNH na mtu anayejitambulisha kuwa Abdallah Said mkazi wa Kitunda Mwanzo, Temeke.

Uchunguzi unaonesha kuwa Said ni baba wa kambo wa Justine ambaye baada ya kumfikisha na kufungua jalada la matibabu, alimsajili kwa jina la Justine Abdallah Said.

Taarifa zilipasha kuwa baada ya kupata taarifa za kifo cha mtoto wake, baba mzazi, Robert Chedega wa Dodoma alijitokeza kutaka kuchukua mwili, lakini alipobaini jina la pili limebalishwa, alisita kufanya hivyo na kuondoka.

Kwa mujibu wa taarifa hizo, Chedega alisema jina sahihi la mtoto wake ni Justine Robert Chedega na kupinga jina alilolikuta akitaka kuchukua mwili alitakiwa kuandika barua maalumu kuomba kibali apewe.

Habari zilipasha kuwa baada ya kuelezwa hivyo na maofisa wa Moi, Chadega alikataa na kuondoka bila kuacha mawasiliano na hadi jana hakuna aliyejitokeza kuchukua mwili wa mtoto huyo.

Baba wa kambo alipotafutwa kupitia namba ya simu aliyoacha MNH kwa kuwa ndiye aliyemfikisha mtoto huyo hospitalini, simu yake haikupatikana.

Ofisa Habari wa Kitengo cha Moi, Jumaa Almasi alipotafutwa ili kupata ufafanuzi wa tukio hilo, simu yake iliita mara kadhaa bila majibu.

Hata hivyo, JAMBO LEO inaendelea kufuatilia tukio hilo kutoka kwa wahusika.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo