Watu 9 mbaroni kwa uvunjaji, wizi


John Banda, Dodoma 

JESHI la Polisi mkoani hapa linashikilia watu tisa kwa tuhuma za uvunjaji nyumba na wizi, huku wakiwa na samani za ndani zinazodhaniwa kuwa za wizi zikiwamo kompyuta mpakato, televisheni na jokofu.

Akizungumza na waandishi wa habari jana, Kaimu Kamanda wa Polisi wa Mkoa, Ernest Kimola, alisema watu hao walikamatwa Novemba 26 na 27   katika msako uliofanywa na Polisi maeneo mbalimbali ya mkoa.

Kamanda alisema kati ya watu hao wanaume ni sita na wanawake watatu wenye umri wa kuanzia miaka 18 ambao walikutwa na televisheni 15, deki 20, redio 10, kompyuta mpakato nane, monita saba za kompyuta, CPU za kompyuta tatu na friji moja. Huku kati yao wakituhumiwa kuwa  wezi, madalali na wanunuzi wa mali za wizi.

Kimola alisema mtandao wa wahalifu hao ni mkubwa kwa kuwa unaunganisha sehemu za masoko ya Morogoro, Dar es Salaam na Mtwara na msako huo unaendelea katika maeneo hayo yote ili kutokomeza mtandao huo.

Alitaja mbinu zinazotumiwa na wahalifu hao kuwa ni kuvunja nyumba usiku au mchana wanapojiridhisha kuwa wenye nyumba hawapo karibu huku wakitumia spana, tindo na mitaimbo kubomoa na kuvunja makufuri.

Aidha, Kamanda alitaka wananchi kujiepusha kununua mali za wizi  zinazouzwa mitaani bila risiti wakishawishika na kuuziwa kwa bei rahisi na katika hali ya kificho na badala yake watoe taarifa Polisi ili watu hao wakamatwe na pia wanaoiba vitu mikoa mingine na kuviuzia mkoa wa Dodoma waache maana wataishia magerezani. 

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo