Wanaotumia ARV kuugua saratani, magonjwa ya moyo


Mwandishi Wetu

WAATHIRIKA wa Ukimwi wanakabiliwa na hatari ya kuugua magonjwa yasiyoambukiza ya saratani na kupata matatizo ya misuli ya moyo, kutokana na athari za matumizi ya Dawa za Kupunguza Makali ya Virusi vya Ukimwi (ARV).

Utafiti mpya uliochapishwa juzi na Taasisi Utafiti wa Saratani na Virusi Vinavyosababisha Ukimwi (VVU) ya Chuo Kikuu cha Califonia, San Francisco (UCSF), umeeleza kuwa saratani hutokea katika tishu za mwili, ambako virusi hivyo hukimbilia kujificha ili visifikiwe na ARV.

Taarifa ya Mtaalamu wa Maabara, Profesa Michael McGrath wa  UCSF iliyochapishwa katika jarida la Virology la mwezi huu, imeeleza     imependekeza utafiti wa haraka ufanyike ili kutafuta muafaka wa tatizo hilo.

Wanasayansi hao wameelezwa kuwa walifanya utafiti huo baada ya kubaini kuwa baadhi ya waathirika wa VVU wanaotumia ARV na kuwa na afya nzuri, hujikuta wakifa ghafla.

“Baada ya kuchunguza tukabaini kuwa vifo hivi vinasababishwa na saratani pamoja na matatizo ya misuli ya moyo,” alisema Profesa McGrath.

Hali hiyo, anasema iliwafanya waendelee na utafiti ambao matokeo yake wameyapata mwezi huu kwa kubaini kuwa virusi vinavyojiviche kwenye tishu za mwili ambako havifikiwi na ARV ndivyo vinasababisha tatizo hilo.

Tangu dawa za ARV zianze kutumika zimeonekana kuzuia VVU kuathiri seli nyeupe za binadamu maarufu kama CD4.

Matumizi hayo yameweza kuwafanya baadhi ya waathirika kupima na kutoonekana tena kuwa na VVU kwenye mfumo wao wa damu lakini wakiacha kutumia ARV huzuka ghafla na kuanza kuonekana vikishambulia CD4.

Profesa McGrath anasema kuwa katika utafiti wao wamebaini kuwa kwenye tishu za mwili wa binadamu ambako VVU hujificha vinasababisha tatizo la saratani na matatizo ya moyo.

“Hivi vifo vya wagonjwa walio katika matumizi ya ARV vinaelekea vinatokana na uwapo wa virusi hawa waliojificha kwenye tishu baada ya kushindikana kufikiwa na dawa ya kuwaangamiza,” alisema Profesa McGrath na akifafanua:

“Utafiti wetu unashauri juhudi zifanyike ili ipatikane dawa ambayo licha ya kuwaangamiza virusi kwenye damu, pia iweze kufika maeneo ambayo virusi hawa hijificha.”

Kwa mujibu wa watafiti wa VVU na Ukimwi, iwapo itapatikana dawa ambayo inawafikia virusi kwenye tishu wanakojificha itakuwa imepatikana dawa kamili.

Kulingana na maelekezo ya matumizi ya ARV kwa sasa, mwathirika wa VVU anapaswa kutumia dawa hizo maisha yake yote.

Hii ni kwa sababu anapoacha virusi hutoka walikojificha na kuanza kusambaa mwilini kwa kuzaliana kwa kutumia CD4 na hii inakuwa rahisi mwathirika kushambuliwa na magonjwa nyemelezi na kuanza kuugua Ukimwi.

Kwa sasa waathirika wanahimizwa kutumia ARV kikamilifu na huu ni mpango endelevu kwa maisha yao yote.

Kutumia kikamilifu kunaweza kufanya hata akipimwa asionekane na VVU kwenye damu na wakati huu huweza kuendelea  na maisha ya kawaida ikiwa ni pamoja na kuoa na kuzaa watoto wasio na maambukizi ya VVU.

Matumizi ya ARV yamewezesha kuwepo na matumaini kwamba VVU ambavyo viligundulika mwanzoni mwa miaka ya 1980, huenda vikavikia ukomo mwaka 2030, iwapo zitatumika vizuri.

Ripoti ya Shirika la Afya Duniani (WHO) inaonyesha kwamba matumizi ya ARV yamepunguza kasi ya maambukizi ya VVU duniani.

Kwa sababu hiyo, mpango wa WHO ni kwamba dunia iwe na maambukizi sifuri ifikapo mwaka 2030, miaka 14 ijayo.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo