Wataka kesi meno ya tembo isiandikwe

Grace Gurisha

UPANDE wa utetezi katika kesi ya Yusuf Yusuf ‘Mpemba’ (34)  umeiomba Mahakama kuzuia kesi hiyo kuripotiwa na vyombo vya habari huku ukidai kuwa mkuu wa nchi anaingilia mwenendo wake na kutaka aache kufanya hivyo kwa sababu iko mahakamani.

Hayo yalidaiwa jana mbele ya Hakimu Mkazi Mwandamizi, Thomas Simba wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Dar es Salaam na Wakili Aloyce Komba wakati kesi hiyo ilipokuja ili kuendelea kusikilizwa, lakini ilishindikana baada ya upande wa Jamhuri kujichanganya katika suala upelelezi.

Komba aliiomba Mahakama itoe tamko la kuzuia kesi hiyo kuripotiwa, kwa sababu vyombo vya habari vimekuwa vikiripoti kinyume na mwenendo wake kwa hiyo washitakiwa wana haki kikatiba kulindwa.

Pia alidai kuwa hata mkuu wa nchi alishatoa toa tamko kuhusu kesi hiyo ilhali anajua washitakiwa wameshakamatwa na wako mahakamani na kesi inaendelea.

“Mkuu wa Nchi nimekuwa nikimsikia akisema kuhusu kesi hii wakati tayari washitakiwa wako mahakamani,” alidai Komba.

Hata hivyo, Hakimu Simba alisema hawezi kutoa zuio la kesi hiyo  kuripotiwa kwa sababu tayari Mahakama ilishawapa haki ya kusikilizwa, kwa hiyo kama kuna chombo kimekosea wanachotakiwa ni kifungua kesi ya madai na si kuzuia.

Kutokana na Wakili Komba kuonekana kutomwelewa vizuri Hakimu na kuendelea kushinikiza zuio litolewe, ilimlazimu Hakimu kutoa darasa kuhusu haki za washitakiwa na vyombo vya habari, hatimaye alikubaliana na alichokisema.

Kabla malumbano hayo hayajatokea, Wakili wa Serikali, Peter Mwita alidai kuwa upelelezi haujakamilika hali iliyomshitua Wakili wa Mpemba, Nehemia Nkoko kwa sababu mara ya kwanza kesi hiyo ilipofika mahakamani, waliieleza Mahakama kuwa upelelezi umekamilika.

Awali, Wakili wa Serikali, Paul Kadushi alidai kuwa upelelezi umekamilika na hivi sasa wanaandaa maelezo ya mashahidi na vielelezo kupeleka Mahakama Kuu Kitengo cha Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi maarufu kama Mahakama ya Ufisadi.

Hakimu Simba alitoa agizo kwa upande wa Jamhuri waweke mipango yao vizuri, na Desemba 15 waieleze Mahakama upelelezi ulikofika na si kutoa taarifa za mgongano.

Mbali na Mpemba ambaye ni mkazi wa Tegeta washitakiwa wengine ni Charles Mrutu (37) wa Mlimba, Morogoro, Benedict Kungwa (40) wa Mbagala Chamazi, Jumanne Chima (30) wa Mbezi, Ahmed Nyagongo (33) na Pius Kulagwa (46).

Washitakiwa hao wanadaiwa kujihusisha na mtandao wa ujangili na biashara ya meno ya tembo yenye thamani ya Sh milioni 785.6.

Ilidaiwa kuwa katika tarehe zisizofahamika kati ya Januari, 2014 na Oktoba, 2016 wakiwa maeneo tofauti ya Dar es Salaam, Tanga, Iringa na Mtwara, walijihusisha na mtandao wa ujangili kwa kukusanya na kuuza nyara za Serikali vipande 50 vya meno ya tembo vyenye thamani ya dola za Marekani 180,000 sawa na Sh milioni 392.8 mali ya Serikali bila kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori.

Aliendelea kudai kuwa katika mashitaka ya pili, Oktoba 26 mwaka huu, washitakiwa wakiwa Mbagala Zakhem, Temeke, walikutwa na vipande 10 vya meno ya tembo vyenye uzito wa kilo 13.85 na thamani ya dola 30,000 (Sh milioni 65.4).

Ilidaiwa katika mashitaka ya tatu, kuwa Oktoba 27, wakiwa Tabata Kisukuru walikutwa na vipande vinne vya meno hayo  vyenye uzito wa kilo 11.1 na thamani ya dola 15,000 (Sh milioni 32.7), huku Oktoba 29 wakikutwa na viapande 36 vyenye thamani ya Sh milioni 294.6 bila kibali cha Mkurugenzi wa Wanyamapori.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo