Waitara ahamishia hasira kwa Makonda


Hajji Kameta, Daystar na Peter Akaro

Mwita Waitara
SIKU chache baada ya wananchi wa Magole ‘A’ Kivule kuvunjiwa nyumba, Mbunge wa Ukonga,  Mwita Waitara amemshutumu Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda kwa kukaa kimya, huku akimwomba Rais John Magufuli kutekeleza mambo makuu mawili ili kutatua mgogoro huo.

Akizungumza Dar es Salaam juzi kwenye mkutano wa hadhara na wananchi hao, Waitara alisema Makonda anaufahamu mgogoro huo tangu akiwa Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni na aliyemkabidhi ofisi ni Jordan Rugimbana baada ya kuteuliwa kuwa Mkuu wa Mkoa wa Dodoma.

“Kwa hiyo walifanya makabidhiano ya ofisi na suala hili lilikuwepo pia, kama walikabidhiwa kuwa hakikisha kuwa watu wa Magole wanapingwa, wanavunjiwa nyumba na asiende kuwasikiliza, hayo ndiyo yalikuwa makubaliano vinginevyo alipaswa awe amekuja hapa,” alisema Waitara.

Aliongeza: “Lakini sasa Makonda amekuwa Mkuu wa Mkoa hivyo yeye na Rugimbana wanazungumza kauli moja, huenda hadi sasa wanapigiana simu kuhusu jambo hili.”

Mbunge huyo alisema anaamini hivyo, kwa sababu kama Makonda alitoka ofisini kwake na msafara wa magari zaidi ya 30 kwenda Gongo la Mboto kumwuliza Mwenyekiti wa Serikali ya Mtaa mapato na matumizi wakati Halmashauri haijawahi kumpa fedha yoyote, jambo ambalo ni dogo, iweje ashindwe kufika walipovunjiwa nyumba wananchi wake kwa mamia.

 “Na mtu ambaye angepaswa kuondoa utata kwa kusema ni Ilala ua Temeke ni Mkuu wa Mkoa, kwa sababu anahusika na wilaya zote, lakini hajafika. Wanaosema nyie ni wa Temeke mbona hadi sasa hawajafika kuwasaidia?” Alihoji.

Aliongeza kuwa hadi sasa hakuna kiongozi wa ngazi ya mkoa ambaye amewahi hata kupiga simu kuulizia hali ya waathirika hao au kutoa pole.

Katika hatua nyingine, Waitara alisema amepata taarifa za chini kwa chini kuwa Rais Magufuli anafuatilia mgogoro huo kwa kutuma watu wake kutafuta taarifa za eneo hilo.

“Namwomba Rais Magufuli mambo mawili; kwanza, atambue hapa kuna matumizi mabaya ya madaraka kwa watu alioteua, kama alitaka kujua angekuja kwa sababu aliowatuma wana maslahi na eneo hili.

“Rais kwa kuwa amekuwa akifika maeneo kwa kushitukiza na kama kuna jambo muhimu Dar es Salaam ambalo anatakiwa kulitumbua majipu na kushitukiza ni hapa Magole Kivule, akifanya hayo mambo mawili atakuwa amewatendea haki Watanzania na masikini wa nchi hii,” alisema Waitara.

Alisema ni vema Rais atambue kuwa wananchi wa Kivule wamekuwa waathirika, kwa sababu wao ni masikini na hawajui sheria, hivyo hahitaji kwenda mikoani, anzie na Dar es Salaam ambako pia kuna watu wanaonewa.

Aliongeza kwamba anafahamu kuwa mgogoro huo ulitengenezwa kwa sababu Rugimbana alikuwa Mwenyekiti wa UVIKIUTA kipindi cha nyuma na walikwenda kwa Mwalimu Julius Nyerere (marehemu) kuomba eneo la kulima na kupewa na ndilo lina utata.

“Lakini hawataki kusema eneo lina ukubwa gani, pia baada ya umri kwenda, Rugimbana amejigeuza kuwa mlezi wa UVIKIUTA na aliwahi kuhojiwa na Mahakama ya Ardhi Temeke kuhusu eneo hili,” alisema.

Waitara aliwaeleza wananchi hao kuwa wameamua kuachana na  wakili aliyekuwa anasimia suala hilo mahakamani, kwani ameshindwa kuomba pingamizi wakati sheria zinaruhusu, amekaa kimya.

Awali mjumbe wa Kamati iliyokusanya misaada kwa ajili ya waathirika, Eliudi Mosire alisoma risala fupi iliyosema kuwa wananchi wengi hawana malazi, makazi, chakula na usalama wao na mali zao ni mdogo.

Wakati akiendelea kusoma risala hiyo, vilio vya akina mama vilisikika mbele ya mbunge wao.

Mosire alisema nyumba zilizovunjwa ni 760, ambazo zilikuwa zikihifadhi watu 540 na sasa kaya 320 hazina pa kuishi, huku kaya 220 zikihifadhiwa kwa ndugu na jamaa.

Kutoka na hali hiyo, watu mbalimbali pamoja na Mbunge walichanga fedha, unga, mafuta, sabuni, sukari na nguo kwa ajili ya kaya 136 ambazo inaelezwa zipo kwenye hali mbaya zaidi.

Maoni

Mkazi wa eneo hilo, Mwanaisha Hamisi alimwomba Rais Magufuli kutembelea eneo hilo na kushuhudia shida wanayopata kwa sasa.

“Aliangalie suala hili, asisikilize maeneo ya kuambiwa, kwa sababu watu wana hali mbaya, tangu tulipovunjiwa watu wanalala nje, watoto hawaendi shule na wengine wamejifungua na hawana sehemu ya kuishi,” alisema.

Mwenyekiti wa Kamati ya Maafa, Abduly Majengo alimpongeza Mbunge huyo kwa kuwaletea misaada, kwani hakuna kiongozi mwingine wa ngazi za juu aliyewaletea misaada.

Asha Mgae alisema licha ya misaada waliropewa na Mbunge, hawaelewi kama wataendelea kuishi katika eneo hilo au watahama.

“Angetakiwa atuweke wazi kabisa, kama tunahama au tutaendelea kuishi hapa, kwa sababu unaweza kujenga chumba kimoja wakavunja tena, mimi sijamwelewa,” alisema.

Ujumbe

Katika mkutano huo, wananchi walibeba mabango yenye ujumbe mbalimbali kuhusu tukio hilo.

Baadhi ulisomeka: ‘Bora kuishi na nyoka ndani kuliko Rugimbana’, ‘Polisi TMK wezi tu’, ‘Rais Magufuli upo au umesafiri?’
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo