Wakuu mikoa 8 washughulikia njaa


Suleiman Msuya

WAKUU wa mikoa minane nchini wamezungumzia ukame na ukosefu wa chakula katika  maeneo yao.

Wakizungumza na gazeti hili juzi, wakuu wa mikoa hao walionesha kuvalia njuga  hali hiyo na kuchukua hadhari.

Waliozungumza ni wakuu wa mikoa ya Pwani, Mwanza, Kilimanjaro, Singida, Iringa, Kigoma, Mtwara na Ruvuma.

Pwani; Everist Ndikilo alisema mkoa wake umetuma wataalamu wa ngazi zote kukusanya taarifa za hali ya chakula na kuahidi kuzungumzia suala hilo hivi karibuni.

“Ni kweli tunaifanyia kazi taarifa hiyo ya kuwepo njaa kwenye mkoa wangu, nimetuma wataalamu ambao watakuja na taarifa ambayo itaonesha hali halisi,” alisema.

Mwanza; John Mongela alisema hana taarifa rasmi ya hali ya chakula mkoani mwake ila ameagiza ngazi ya wilaya, kata na vijiji kutoa taarifa na Jumanne ijayo, atakuwa na taarifa sahihi.

Mongela alisema ni kweli zipo taarifa za njaa ila ni vigumu kubainisha hali halisi ilivyo kabla ya kupata taarifa sahihi.

Kilimanjaro; Saidi Sadick alisema baada ya mavuno ya mwaka jana walipata akiba ya zaidi ya tani 63,000 lakini kutokana na biashara huria upo uwezekano wa kiasi hicho kupungua.

Alisema wapo wafanyabiashara waliokuwa wanapitisha mazao kwa njia za magendo wilayani Rombo, hali ambayo inaweza kuchangia upungufu wa chakula.

“Sisi tunatoa elimu kwa wananchi, ili kutunza mazao na kama wameishiwa chakula wauze hata mifugo, wanunue kwani hali ya mvua haitabiriki kwa sasa,” alisema.

Singida; Dk Rehema Nchimbi alisema mkoa wake ulivuna zaidi ya tani 762, 202 ambapo mahitaji ni tani 435,125 hivyo kubaki na ziada ya zaidi ya tani 300,000.

Nchimbi alisema pamoja na mavuno hayo, wakulima wengi waliuza mazao hayo hali ambayo inaweza kuchangia ukosefu wa chakula kwa siku za karibuni.

“Tumetuma wataalamu wetu kwenye baadhi ya wilaya ambazo kimsingi zimekuwa zikikabiliwa na changamoto ya chakula kama Itigi, Manyoni, Mkalama na Iramba hapo tutapata hali halisi ya chakula,” alisema.

Iringa; Amina Masenza alisema mkoa wake ulikuwa na akiba kidogo, hivyo ni dhahiri kuwa upo uwezekano wa changamoto ya chakula kutokea.

Alisema mkoa wake umevamiwa na wafanyabiashara, hali ambayo inaweza kuchochea upungufu huo, huku akitaka wananchi kuhifadhi chakula na kulima mazao ya muda mfupi.

Kigoma; Brigedia Jenerali mstaafu Emmanuel Maganga: “Katika mkoa wa Kigoma hatuna historia ya njaa, kwa sababu ardhi yetu ina rutuba hivyo siwezi kufikiria kuwa njaa itatokea, kwani mvua zimeanza na wakulima wako mashambani.

Alisema mwaka jana walivuna zaidi ya tani milioni 1.1 huku mahitaji ya mkoa yakiwa ni zaidi ya tani 500,000 hivyo kuwa na ziada ya zaidi ya tani 590,000.

Alsema wananchi wake wamekuwa wakiuza mazao yao mikoa ya jirani ikiwa ni pamoja na kujihusisha na kilimo cha muda mfupi, hivyo kujihakikishia chakula kila siku.

Mtwara; Halima Dendegu alisema mkoa wake ulivuna tani zaidi ya 875,000 ambapo mahitaji kwa mwaka ni zaidi ya tani 460,000 hivyo kuwa na ziada ya zaidi ya tani 400,000.

Alisema pamoja na mavuno hayo, wamekuwa wakisisitiza wananchi kulima mazao kama muhogo, ambayo yanahimili ukame na kuhifadhi fedha za mauzo ya korosho ili ziwasaidie kununua chakula.

Ruvuma; Dk Binilith Mahenge alisema mkoa wake hauna uhaba wa chakula na kuwa katika mavuno ya mwaka jana, walipata zaidi ya tani 850,000 ikilinganishwa na mahitaji ya zaidi ya tani 400,000 kwa mwaka hivyo kuwa na ziada ya tani 400,000.

Alisema kiasi hicho cha zaidi ya tani 800,000 ni kwa mazao ya mahindi pekee ila kwa ujumla wa mazao yote, walivuna zaidi ya tani milioni 1.7.

Manyara; Dk Joel Bendera alisema mkoa wake una maeneo ambayo ukame ulikuwa mkubwa, hali ambayo inaweza kuhatarisha upatikanaji wa chakula.

Bendera alisema mikakati ya mkoa wake ni kuhamasisha kila mwananchi anatunza chakula alichonacho ili hali ikiwa mbaya zaidi aweze kukabiliana nayo.

“Hali ya mabadiliko ya tabia nchi inatishia usalama wa chakula hasa ukizingatia mkoa wa Manyara unategemea Hanang, Babati na Mbulu, hivyo tunahamasisha kilimo cha muda mfupi,” alisema.

Tabora; Aggrey Mwanri alisema hali ya chakula mkoani mwake ni nzuri kiasi na kuwa wanachofanya sasa ni kuhamasisha kilimo cha kisasa.

“Hofu kubwa inatokana na mabadiliko ya tabianchi ambayo yamekuwa yakitokea kwa kasi kubwa hivyo kinachohitajika ni wananchi kulima kilimo cha muda mfupi,” alisema.

Jitihada za JAMBOLEO kupata wakuu wa mikoa mingine zilishindikana kwa baadhi yao simu zao kuita bila kupokewa huku za wengine zikiwa hazipatikani.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo