Suala la mizigo ya WAMA laitesa TRA


Suleiman Msuya

TAASISI ya Wanawake na Maendeleo (WAMA) yaitesa TRA. Hivyo ndivyo unavyoweza kusema kutokana na taarifa ya mizigo ya taasisi hiyo kudaiwa kuzuiwa bandarini hadi ilipe kodi, kuandikwa na vyombo mbalimbali.

Siku chache baada ya Ikulu kukanusha taarifa hizo zilizodai Rais John Magufuli anahusika kuzuia mizigo hiyo, Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), imesisitiza kuwa taarifa hizo hazikuwa za kweli.

Kupitia Kamishna Mkuu, Aliphayo Kidata jana TRA ilikanusha taarifa hizo ikisema orodha iliyochapishwa na baadhi ya magazeti nchini ikijumuisha jina la WAMA haikuwa sahihi.

Kidata alisema WAMA iliingiza nchini makasha 11 ya vitabu na kamusi kutoka Japan kwa ajili ya matumizi ya elimu.

“Kwa mujibu wa Sheria ya Forodha ya Afrika Mashariki ya 2004, pamoja na Sheria ya Ongezeko la Thamani (VAT) ya mwaka 2015 vitabu hivyo havitozwi kodi ya forodha wala VAT,” alisema Kidata. 

Alisema vitabu hivyo vilitozwa tozo ya uondoshaji mizigo bandarini Sh 42,483 na ya Maendeleo ya Reli Sh 106,438 ikiwa ni jumla ya Sh 148,921.

“Baada ya malipo hayo kufanyika, vitabu hivyo vilichukuliwa na WAMA tangu Agosti 10,” alisema.

Alisema taarifa zilizoandikwa na baadhi ya magazeti hivi karibuni juu ya vitabu hivyo kuwa kwenye orodha ya bidhaa zinazopaswa kupigwa mnada kwa sababu ya kutolipiwa kodi haikuwa sahihi.

Kamishna huyo alisema vitabu hivyo havikupaswa kutozwa kodi ya forodha wala VAT kwa mujibu wa sheria, hivyo WAMA haikupaswa pia kuomba msamaha wa kodi kwenye mamlaka yoyote. 

Desemba 4 Ikulu kupitia Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais ilitoa taarifa za kukanusha Rais Magufuli kuhusika kuzuia mizigo hiyo bandarini mpaka hapo itakapolipiwa kodi.

“Tunapenda kuutarifu umma kuwa taarifa hizo si za kweli na ni uzushi, kwani Rais Magufuli hajawahi kuzuia wala kuagiza kuzuiwa kwa mizigo ya Mama Salma Kikwete,” ilisema taarifa.

Taarifa hiyo ilisema Rais Magufuli alisikitishwa na uzushi huo unaofanywa kwa lengo la kumchafua Rais mstaafu, Jakaya Kikwete na familia yake.

“Nimesikitishwa sana na uzushi unaofanywa dhidi ya Rais mstaafu Dk Kikwete na mke wake Mama Salma, tafadhali mnaotengeneza uzushi huu acheni mara moja na mwacheni Rais mstaafu Kikwete apumzike,” ilisema taarifa hiyo.

“Rais mstaafu Kikwete amefanya kazi kubwa ya kulitumikia Taifa hili, amestaafu anapumzika, narudia mwacheni apumzike, Serikali haitaendelea kuvumilia uzushi na uchonganishi huu unaofanywa kwa makusudi ili kuchafua viongozi wastaafu,” Rais Magufuli alikaririwa akionya.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo