Bilioni 130/- kuboresha bandari Dar


Sharifa Marira

MAMLAKA ya Usimamizi wa Bandari Tanzania (TPA) inatarajia kutumia Sh bilioni 132 kukarabati bandari ya Dar es Salaam kwa kuboresha miundombinu ili iweze kupokea mizigo mingi.

Ukarabati huo utasaidia kuiinua Bandari hiyo inayopokea mizigo inayoingia nchini kwa asilimia 90 hadi 95 ukitokana na msaada wa fedha kutoka Serikali ya Uingereza kupitia Taasisi ya Trade Mark East Africa (TMEA).

Hatua hiyo inatajwa kumsaidia Rais John Magufuli kufikia malengo yake kuinua uchumi wa Taifa na kuwa nchi ya kipato cha kati, kutokana na ukweli, kwamba baada ya ukarabati huo Bandari hiyo itakuwa na uwezo wa kuchukua mizigo mikubwa zaidi ya bandari zingine za nchi jirani.

Kwa mujibu wa TPA, kazi ya ukarabati inatarajiwa kuanza mara moja baada ya jana kusaini mkataba wa makubaliano na Taasisi ya Trade Mark East Afrika (TMEA) tawi la Tanzania.

Akizungumza wakati wa kusaini mkataba huo, Mkurugenzi Mkuu wa TPA, Deusdedit Kakoko alisema ukarabati huo ni mkubwa na lango lote la Bandari litafumuliwa na kazi hiyo itakamilika ndani ya miaka minne ijayo.

Alisema kwa sasa wanapitisha meli za tani milioni 15, lakini baada ya uboreshaji huo watapokea meli za tani milioni 26.

“Tumetafuta wakandarasi na kuna Mchina anaonekana kushinda, kama akipita tutaanza mradi mara hivyo itakwenda haraka na itakuwa nzuri, ikifika mwaka 2019 na 2020 tuna imani kila kitu kitakuwa sawa,” alisema Kakoko.

Alisema baada ya uboreshaji, TPA itaendelea kuboresha bandari zingine ikiwamo ya Bagamoyo ili kusaidiana na ya Dar es Salaam.

Mkurugenzi wa TMEA Tanzania, John Ulanga alisema fedha hizo si mkopo bali ni msaada kwa Serikali na endapo mradi huo utakwenda vizuri na kukamilika mwaka 2019 kuna uwezekano  wa kuomba fedha kwa ajili ya bandari zingine ikiwamo ya Kigoma.

Alisema TMEA wana miradi mingi ya kuboresha mazingira ya kibiashara na wanaboresha bandari hiyo kutokana na umuhimu wake, kwani asilimia 40 ya kodi inapatikana kupitia bandari hiyo.

“Tunaishukuru Uingereza ambayo imetoa msaada huu na kupitia kwetu tumeleta hapa TPA katika mradi huu mkubwa ambao utaleta mabadiliko chanya ya kushindana na bandari zingine ikiwamo ya Mombasa, Kenya,” alisema Ulanga.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo