Mti mrefu Afrika waonekana Kilimanjaro


Mwandishi Wetu

MTI mrefu kuliko yote barani Afrika wenye urefu wa meta 81.5 na umri unaokadiriwa kuzidi miaka 600, umegundulika Tanzania katika bonde nje ya Hifadhi ya Mlima Kilimanjaro (Kinapa).

Ugunduzi huo ni wa mtafiti wa Chuo Kikuu cha Bayreuth, Ujerumani, Andreas Hemp na kutangazwa hivi karibuni, baada ya kufanya utafiti wa uoto wa asili katika hifadhi hiyo miaka 20 iliyopita.

Hata hivyo, kwenye utafiti huo miaka hiyo, hakufanikiwa kufika eneo ulipo mti huo unaotajwa kuwa aina ya Entandrophragma excelsum, kutokana na umbali na tekinolojia aliyokuwa nayo hadi mwaka 2012 aliporejea kufanya kutafiti tena, akiwa na jopo la watafiti wenzake na teknolojia ya kisasa ya kupima urefu wa miti.

Taarifa iliyochapishwa kwenye mtandao wa Mother Nature Network (MNN) Novemba 27, ilieleza kuwa Hemp akishirikiana na jopo la watafiti hao wa chuo hicho, waligundua mti huo.

Katika utafiti huo, watafiti walipima miti 32 kati ya mwaka 2012 na mwaka huu kwa teknolojia ya kisasa, wakapata miti 10 yenye urefu unaoanzia meta 59.2 na kufanikiwa kupata huo wa meta 81.5, ambao ndio huo ulioweka rekodi ya Afrika.

Kabla ya ugunduzi huo, mti uliokuwa ukishika rekodi hiyo ni aina ya Sydney blue gum (Eucalyptus saligna) uliokuwa Limpopo, Afrika Kusini, ambao hata hivyo ulianguka mwaka 2006.

Inadaiwa kuwa mti mrefu kuliko yote duniani uko California, Marekani wenye meta 115.7 na wa pili uko Tasmania, Australia, ukiwa na meta 99.8.

Mti wa tatu kwa urefu uko California pia, una meta 94.9, ukifuatiwa na wa nne ulioko Tasmania, wenye urefu wa meta 89.0. Wa tano kwa urefu uko kisiwa cha Mindanao, Ufilipino na wa sita kwa urefu duniani ndio huo wa Tanzania.

Ilielezwa kuwa Afrika hakuna taarifa za uwepo wa miti mingi mirefu na yenye umri mrefu, kutokana na upungufu wa utafiti katika Bara hilo, unaosababisha miti mingi kutofanyiwa vipimo na hali ya umasikini wa Bara hilo, unaochangia miti mingi kukosa fursa ya kurefuka.

Hata hivyo, hali hiyo inaelezwa kutokuwapo Kinapa, ambayo ina udongo wenye rutuba inayotokana na asili ya volcano, unaoelezwa kuchangia kukua kwa mti huo.

“Ni kama Jiji katikati ya msitu,” alisema Hemp, alipokuwa akielezea mazingira ya mti huo na mingine iliyofanyiwa vipimo.

Hemp alitaja sifa nyingine iliyochangia kurefuka kwa mti huo kuwa ni kuwa mbali na wakataji magogo, ambao wamekuwa wakiharibu mazao ya misitu kwingineko.

Hata hivyo, mtafiti huyo alihadharisha kuwa miti hiyo iko nje ya mpaka wa Kinapa, hali inayoonesha kuwa bado iko hatarini na kueleza matarajio yake, kuwa ugunduzi huo huenda ukasababisha kuongezwa kwa mipaka ya hifadhi hiyo, ili kulinda mti huo.

Ni jukumu la Serikali na vyombo vyake na wananchi kuilinda hazina hiyo ambayo inaweza kuchangia mapato kupitia sekta ya utalii.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo