ATCL njia nyeupe Serikali kununua ndege mpya tatu


Mwandishi Wetu

SHIRIKA la Ndege la Tanzania (ATCL) limeanza kuachiwa soko la usafiri wa anga, baada ya mashirika pinzani kufuta safari za baadhi ya maeneo, huku Serikali ikitajwa kumaliza kusaini ununuzi wa ndege mpya tatu.

Taarifa zilizopatikana jana, zilieleza kuwa Tanzania imeingia makubaliano ya ununuzi wa ndege tatu mpya zinazotengenezwa na kampuni ya Bombardier ya Canada, ikiwemo moja aina ya Q400NG, inayofanana na mbili zilizozinduliwa na Rais John Magufuli, Septemba.

Kwa mujibu wa taarifa hizo kutoka Bombardier, ambazo ziliripotiwa kwenye mitandao ya kijamii jana, ndege zingine mbili ni aina ya CS300, ambazo ni toleo jipya la ndege za Bombardier na kila moja ina uwezo wa kubeba abiria kati ya 100 na 150.

Ndege hizo aina ya CS300, zinatajwa kuongoza kwa sifa ya matumizi madogo ya mafuta kwa safari ndefu, ambazo zinatarajiwa kufufua safari za ATCL katika nchi mbalimbali za Afrika na nje ya Afrika.

Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Tanzania ndiyo nchi ya kwanza kuagiza CS300 katika nchi za Afrika, baada ya hivi karibuni kampuni hiyo kuuza ndege hizo kwa Shirika la Ndege la Baltic na Swiss, ambayo ni mashirika yaliyo chini ya mwavuli wa Kundi la Mashirika ya Ndege ya Lufthansa.

Hivi karibuni, Rais Magufuli akizungumza na wahariri wa vyombo vya habari, Ikulu Dar es Salaam, aliahidi ununuzi wa ndege hizo ambapo alisema alishalipia asilimia 30 na zinatarajiwa kufika nchini mwanzoni mwa mwaka 2018.

Rais Magufuli alitaja pia mpango mwingine wa kununua ndege aina ya Boeing, yenye uwezo wa kubeba abiria 242, ambayo kabla ya mchakato wa ununuzi kuanza, Serikali ilitakiwa kulipa dola za Marekani milioni 10, ambazo zimeshalipwa, hivyo mazungumzo ya awali yangeanza.

Taarifa ya jana ilieleza kuwa ndege inayozungumzwa ni aina ya Boeing B787 Dreamliner, ambayo mazungumzo ya ununuzi wake yameanza.

Inatarajiwa ununuzi wa ndege hizo, utasaidia ATCL kuanza safari za nje ya Afrika, baada ya Bombardier Q400NG, zilizopo nchini kuanza safari za baadhi ya nchi jirani.

Kuachiwa soko

Ununuzi huo wa ndege mpya umetajwa kufanyika kwa wakati mwafaka, wakati washindani katika biashara ya usafiri wa anga, Precision Air na Fastjet, wakitangaza kupata hasara na kupunguza safari za baadhi ya miji, huku hatua za kuahirisha safari zikichukuliwa mara kwa mara.

Miongoni mwa masoko ambayo imeelezwa kuwa ATCL ni kama imeanza kuachiwa ni pamoja na za  Dar es Salaam- Entebbe na Nairobi, ambazo wachambuzi wa mambo walieleza kuwa ni soko ambalo halikutarajiwa, lakini linaloweza kukamatwa na shirika hilo kwa kutumia ndege zake ndogo, ambazo zina sifa ya matumizi madogo ya mafuta.

Hatua hizo za ATCL zilifananishwa na zinazochukuliwa na Serikali ya Rwanda kupitia RwandAir, ambayo imeamua kununua ndege mbili aina ya Airbus A330.

Hata hivyo, ilielezwa kuwa hali hiyo huenda ikazorotesha jitihada za kufufua Air Uganda kwa kuwa soko la Afrika Mashariki, limeanza kujaa kutokana na nguvu za Shirika la Ndege la Kenya (KQ).

Ilielezwa kuwa kuibuka kwa RwandAir inayoonekana kuwa shirika linalojiamini na linalokua kwa kasi kiasi cha kuhudumia Uganda na kufufuliwa kwa ATCL, ambayo huenda ikapata zaidi ya ndege mpya sita, ikijumlishwa na tatu zilizopo, kunafanya biashara hiyo ya usafiri wa anga kuwa na ushindani utakaoathiri kampuni mpya za usafiri wa anga.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo