Mashinji: Wanaozuia siasa wana upofu


Suleiman Msuya

Dk Vincent Mashinji
KATIBU Mkuu wa CHADEMA, Dk Vincent Mashinji, amesema changamoto wanazokutana nazo katika kufanya siasa zinatokana na upofu wa viongozi wanaowazuia.

Wakati Mashinji akieleza hayo, Mwenyekiti wa Chama hicho, Freeman Mbowe ameanza ziara ya kikazi ya siku 14 Ulaya kuwakilisha chama kwenye Mkutano Maalumu wa Vyama vya Kidemokrasia Duniani.

Akizungumza jana na JAMBOLEO, Mashinji aliweka bayana kuwa pamoja na zuio la mikutano ya hadhara, bado wapo watendaji na viongozi wasiojiamini hivyo kubana demokrasia.

Mashinji alisema moja ya mikakati yao kipindi hiki ni kufanya siasa za kujenga chama kimfumo na kuachana na siasa za kiuanaharakati hivyo uamuzi huo wa kuwazuia haujaathiri jambo lolote kichama.

“Yapo mafanikio makubwa sana kutokana na mfumo wa siasa ambazo tunazifanya na zimeanza kusumbua watawala, hali ambayo inasababisha kila kukicha wanaibuka na mikakati mipya ya kukabiliana nasi,” alisema.

Katibu Mkuu huyo alisema siasa ni mchakato unaokutana na vikumbo vingi, hivyo wao wamejipanga kukabiliana navyo hatua kwa hatua.

Alisema jambo la kupongeza ni wananchi wamewaelewa watawala kuwa ni watu wa aina gani, hivyo hawapati shida ya kufanya nao kazi za kila siku.

Mashinji alisema kila kukicha wanabuni mbinu mpya ya kufikia wananchi na kuwafikishia ujumbe, hivyo mikakati ya Serikali na chama kuwakabili haiwezi kufua dafu.

“Unajua mikutano ya ndani imekuwa ikitoa matokeo chanya kwa wanachama wetu, hivyo naamini ikiendelea hivi hivi ni hatua nzuri katika chama,” alisema.

Tangu Rais Magufuli aingie madarakani, vyama vya siasa nchi vimekuwa katika hali ngumu ya kufanya siasa, hali ambayo imekuwa ikiibua malalamiko kutoka pande mbalimbali za nchi, huku wengine wakiona kama ni mkakati wa Serikali kuua vyama vya upinzani.

Katika matamko na kauli za viongozi wa Serikali wakiongozwa na Rais, wamekuwa wakisema waachwe wafanye siasa na siasa zitaanza mwaka 2020 jambo ambalo ni kinyume na Katiba na Sheria ya Vyama vya Siasa, ambayo inataka vyama vifanye siasa.

Katazo hilo limesababisha wanachama na viongozi wa vyama vya siasa wakizuiwa kufanya mikutano na wengine kushikiliwa na Polisi kwa muda ambapo kwa siku za karibuni, hali hiyo ilimkumba Katibu Mkuu wa CUF, Maalim Seif Sharif Hamad na baadhi ya viongozi wa Chadema.

Kwa upande mwingine, Msemaji wa Chadema, Tumaini Makene alisema Mbowe anaongoza wajumbe wa chama hicho kwenye mkutano huo ambamo atapata nafasi ya kuhutubia.

Alisema katika ziara hiyo yumo Mwanasheria Mkuu wa Chadema, Tundu Lissu na Mkurugenzi wa Mambo ya Nje na Mawasiliano, John Mrema na utazuru pia Ujerumani, Uingereza na Ubelgiji yaliko Makao Makuu ya Jumuiya ya Ulaya (EU).

Makene alisema akiwa London, Mbowe na ujumbe wake watakutana na viongozi wa Serikali, wabunge, ujumbe maalumu wa Jumuiya ya Madola na wawakilishi wa taasisi mbalimbali za kimataifa.

“Mjini Brussels (Ubelgiji), atapata fursa ya kuonana na kufanya mazungumzo na viongozi wa  EU na taasisi zake,” alisema.

Makene alisema wajumbe kutoka nchi mbalimbali watazungumza na kubadilishana uzoefu kuhusu demokrasia, mafanikio na changamoto katika maeneo yao na dunia kwa ujumla.

Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo