Mama Maria Nyerere |
MJANE wa Baba wa
Taifa, Mwalimu Julius Nyerere, Mama Maria Nyerere, ameipongeza Serikali kwa
namna inavyotoa kipaumbele kwenye sekta ya elimu chini ya mpango wa elimu bure,
hivyo kuongeza nafasi na hadhi ya mwanamke katika jamii.
Mama Maria alitoa pongezi hizo kwenye mahojiano maalumu kuhusu maadhimisho ya miaka 55 ya Uhuru nyumbani kwake Mikocheni, Dar es Salaam jana.
“Elimu imebadili
nafasi ya mwanamke katika jamii, tukiangalia wakati tunapata uhuru wanawake
wengi walikuwa bado hawajui kusoma na kuandika,” alisema Mama Maria.
Aliongeza kuwa
wakati Tanzania ikipata Uhuru mwaka 1961 idadi ya wanawake walioshika nafasi za
uongozi walikuwa wachache na hazikuwa nafasi kubwa, jambo ambalo ni tofauti na
sasa, kwani kwa mara ya kwanza Tanzania ina Makamu wa Rais mwanamke, Samia
Suluhu Hassan.
Alisema pamoja na changamoto zilizopo, Serikali za awamu zote zilijitahidi kuhakikisha zinapiga hatua za kukabiliana na adui ujinga.
Kwa mujibu wa
Mama Maria ni faraja kwa Serikali ya sasa kutambua umuhimu wa watoto kwenda
shule kwa kutoa elimu ya bila ada, kwani hiyo inasaidia kupunguza watoto wa
mitaani.
“Elimu imeleta ukombozi, watoto waliokuwa hawaendi shule walikuwa wanaingia makundini ndipo unasikia Panya Road, mbwa mwitu na mengine,” alisema Mama Maria.
Aidha, alisema
ili Taifa lipate maendeleo ni lazima kujiamini, kuthubutu na kutenda kama
ambavyo sasa Serikali imejiamini na kuonesha uthubutu katika falsafa ya Hapa
Kazi Tu na Tanzania ya Viwanda.
Mama Maria alitoa rai kwa wanawake kushirikiana kuhakikisha wanatunza viwanda vinavyojengwa ili kuwa chachu ya maendeleo ya Taifa na jamii kwa ujumla.
0 comments:
Post a Comment