Viwanda 400 kushiriki maonesho ya viwanda Dar


Mwandishi Wetu
                  
Frank Kanyusi
ZAIDI ya viwanda 400 vinatarajia kushiriki maonesho ya viwanda nchini, lengo likiwa ni kutangaza na kukuza sekta ya viwanda na kuiwezesha kuchangia ukuaji wa uchumi wa Taifa.

Maonesho hayo yanatarajia kuanza leo hadi Desemba 11 kwenye Uwanja wa Maonesho ya Biashara ya Kimataifa wa Mwalimu J.K Nyerere, Dar es Salaam.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Usajili wa Biashara na Leseni (BRELA), Frank Kanyusi, alisema jana Dar es Salaam kwamba maonesho hayo yanalenga kutekeleza azma ya Serikali ya kuifanya Tanzania kuwa nchi ya viwanda.

“Maonesho hayo yatatoa fursa kwa viwanda vidogo, vya kati na vikubwa, kuonesha bidhaa wanazozalisha nchini na pia kutoa hamasa kwa Watanzania kutumia bidhaa hizo,” alisema Kanyusi.

Alifafanua: “Tunataka wazalishaji kwenye viwanda vya chini hadi vikubwa, waje waoneshe Watanzania kinachozalishwa, huku tukitarajia wananchi watahamasika kununua bidhaa hizi zinazozalishwa Tanzania.”

Alisema tukio hilo linalojumuisha wazalishaji, wafanyabiashara na wananchi ni fursa nzuri ya kutoa huduma zinazohusu uwekezaji kwenye sekta ya viwanda na biashara, zitakazopatikana kwenye viwanja vya maonesho na kutolewa na watendaji wa BRELA.

“Hii ni fursa pia kwa washiriki na wananchi kupata huduma za haraka, za papo kwa papo zinazohusu sekta za viwanda na biashara. Huduma hizo ni pamoja na usajili wa kampuni, alama na majina ya biashara, utoaji leseni za viwanda na urasimishaji wa biashara," alisema Kanyusi.

Alisema BRELA itakuwa na banda maalumu litakalotoa huduma kwenye viwanja hivyo na alitaka washiriki na wananchi wengine wenye kuhitaji huduma za usajili au leseni za viwanda vidogo na vikubwa, kutumia maonesho hayo kupata huduma nyingi zitakazotolewa muda wote wa maonesho hayo.

Akizungumzia urasimishaji wa biashara, Kanyusi alisema ni wakati mwafaka kwa Watanzania kufanya urasimishaji wa biashara zao, kwa lengo la kuwafanya waendeshe au wamiliki biashara halali na inayotambulika kisheria, hivyo kuwaondolea usumbufu usiokuwa wa lazima kutoka kwenye taasisi na vyombo vya Serikali.

Maonesho hayo yameandaliwa na Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE) kwa kushirikiana na wadau  likiwamo Shirika la Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNIDO), Shirika la Maendeleo ya Viwanda Vidogo  (SIDO), Shirika la Viwango Tanzania (TBS) na Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).

Washiriki wengine wa maandalizi ya  maonesho hayo ni Shirika la Maendeleo Tanzania (NDC),  Ukanda Huru wa Uwekezaji (EPZA), Mamlaka ya Chakula na Dawa (TFDA), Kituo cha Uwekezaji Tanzania (TIC), Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Kampuni inayojihusisha na alama za biashara ya GSI na wadau wengine kutoka Zanzibar.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo