Lowassa: Tutashinda uchaguzi wa 2020


*Apongeza mikutano ya hadhara ya kisiasa kuzuiwa
*Asema ya ndani imekuwa ‘mitamu’, imewaimarisha

Sharifa Marira

Edward Lowassa
MJUMBE wa Kamati Kuu ya Chadema, Edward Lowassa, amesema kwa hali ilivyo na inavyoendelea nchini kuna kila dalili za chama hicho kushinda uchaguzi mkuu mwaka 2020.

Aidha, Lowassa amesema mikutano ya ndani ambayo imeruhusiwa na Rais John Magufuli ni ‘mitamu’ zaidi na anashukuru kwa kiongozi huyo kuzuia mikutano ya nje, kwani ya ndani imesaidia kuwajenga zaidi kwa kuonana ana kwa ana.

Lowassa alisema hayo jana Dar es Salaam, wakati kuna kilio kikubwa cha wananchi wanaolia kukabiliwa na hali ngumu ya kiuchumi, huku wengi wakidhani imesababishwa na kubana matumizi kunakofanywa na Serikali.

Alisema hayo wakati akifungua semina kwa wabunge, mameya na madiwani wa chama hicho wa Jiji la Dar es Salaam ikilenga kujadili kazi waliyofanya ya kutumikia wananchi kwa mwaka mmoja na namna ya kupiga hatua miaka minne ijayo.

Alifafanua: ”Nimepita maeneo mengi kufanya mikutano ya ndani, kwa hali ilivyo tunakubalika mno, tuna dalili zote za kushinda uchaguzi mkuu wa 2020, tujitahidi kuwa na umoja, bila umoja hatuwezi kushinda ni muhimu sana, CCM wanajua maana ya umoja na wanaung’ang’ania, tuangalie sana maneno ya kutugawa tusiyakubali.’’

Alisema Chadema itapita maeneo ambayo watu wako nyuma kielimu ambayo kwa kiasi kikubwa wameipigia kura CCM, ili kuwaelewesha nia njema ya kuwaletea maendeleo na kuwapa elimu.

‘’Muda uliobaki ni mchache, tunatakiwa kuamka ili chama chetu kishinde kwa kuwa tumeshakifikisha sehemu nzuri, hatuna muda tuchangamke kila mmoja aone kwamba anapaswa kueleza namna ya kukisaidia chama kivuke,’’ alisema Lowassa.

Kuhusu mikutano ya ndani ambayo aliita ‘mitamu’ zaidi, alisema vimefanya wamekuwa imara zaidi, kwani wamezungumza na wanachama wao maeneo mengi wakiwa wanaonana kwa karibu.

‘’Tumekuwa mikoani na viongozi wenzangu, tumezunguka mikoani hali ni nzuri kwa mazungumzo tuliyofanya na wanachama wetu, vikao ni vitamu zaidi kuliko vya nje, unapata nafasi ya kuongea na wananchi ana kwa ana kwa muda mrefu, kwa mapenzi na mahaba yote,’’ alisema Lowassa.

Lowassa aliwataka mameya na viongozi wengine wa Chadema jijini humo kukataa kutoa mikataba ya aina yoyote kienyeji na kushughulikia suala la maegesho, ili isifike mahali wananchi wakajuta kuichagua Chadema na kusema afadhali CCM.

Zabuni ya maegesho jijini Dar es Salaam imetolewa kwa kampuni ya Kenya ambayo imeongeza tozo ya kuegesha gari kutoka Sh 300 hadi Sh 500 kwa saa.

Alisema kero ambayo wamekuwa wakikutana nayo katika mikutano yao ni wananchi kutaka uongozi, jambo ambalo alisema kama ingepatikana Katiba mpya zingeongezwa nafasi zaidi za kuteuliwa.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo