CCM kujadili mambo mazito Dar


Fidelis Butahe na Charles James

Christopher ole Sendeka
MWENYEKITI cha CCM, Rais John Magufuli ameitisha kikao cha Kamati Kuu (CC) na Halmashauri Kuu ya Taifa (NEC) ya Chama hicho vitakavyofanyika kwa siku tatu Dar es Saalam huku wachambuzi wakibashiri ajenda kadhaa zitakazoibuka katika vikao hivyo.

Katika kuonesha umuhimu wa vikao hivyo pamoja na ajenda ya Rais Magufuli kubana matumizi kwa kutosafiri, mkutano NEC ya CCM utafanyika Dar es Salaam badala ya Dodoma kama ilivyozoeleka.

Ajenda zinazotajwa kuibuka katika vikao hivyo ni maandalizi ya uchaguzi mdogo wa ubunge katika Jimbo la Dimani, Zanzibar na madiwani katika kata 22 kwenye halmashauri 21 Tanzania Bara, mabadiliko ya sekretarieti ya chama hicho inayoongozwa na Katibu Mkuu, Abdulrahman Kinana na utendaji kazi wa Serikali iliyoko madarakani.

Nyingine ni madeni ya chama hicho yaliyotokana na kampeni za uchaguzi mkuu mwaka jana na kuunda Bodi na Menejimenti ya Uhuru Publications Limited (UPL) inayochapisha magazeti ya Uhuru, Mzalendo na Burudani.

Taarifa iliyotolewa jana na Seleman Mwenda kwa niaba ya Msemaji wa Chama hicho, Christopher ole Sendeka, ilieleza kuwa kikao cha CC kitafanyika kwa siku mbili, Desemba 11 na 12 na kufuatiwa na  cha NEC, huku ikihimiza wajumbe wote wa vikao hivyo kuhudhuria.

Tayari vyama vya siasa vimepewa barua kuhusu marudio ya uchaguzi wa ubunge Dimani Januari 22 kutokana na kifo cha aliyekuwa Mbunge wake, Hafidh Ally Tahir huku kampeni zikitarajiwa kuanza Desemba 23 na kumalizika Januari 21.

Aidha, uamuzi wa Rais Magufuli kuwateua Dk Emmanuel Nchimbi,  Dk Pindi Chana na Dk Asha-Rose Migiro (wote wajumbe wa Kamati Kuu) na Rajab Ruhwavi ambaye ni Naibu Katibu Mkuu wa CCM, Bara, kuwa mabalozi, unaashiria chama hicho kuanza mchakato wa kusaka makada wa kuziba nafasi hizo na pengine kuunda upya Sekretarieti ya chama hicho.

Akizungumzia vikao hivyo, Dk George Kahangwa wa UDSM alisema: “Naona utakuwa mjadala wa kujaza nafasi zilizo wazi. Pia ahadi za Rais Magufuli alizotoa kwenye kampeni pia zitajadiliwa, sambamba na alizotoa wakati akikabidhiwa uenyekiti wa chama, ikiwamo ile ya kufuta chipukizi.

“Uchaguzi wa ndani wa chama hicho lazima utajadiliwa pia, pongezi huenda zikatolewa kwa Serikali ya Awamu ya Tano ambayo inaonekana kuwa tofauti na zilizopita, sambamba na kupima utendaji kazi wa baadhi ya mawaziri,” alisema.

Katika ufafanuzi wake, Dk Kahangwa alisema chama hicho tawala kinapaswa kujadili hali ya siasa nchini kutokana na kuminywa kwa demokrasia, akitolea mfano wa kuzuiwa kwa mikutano ya hadhara,

“Wajitathmini pia kwa kile kilichotokea Zanzibar kwenye Uchaguzi Mkuu,” alisema.

Mhadhiri wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM), Dk Benson Bana alisema: “Suala la uchaguzi mkuu wa CCM linaweza kujadiliwa katika vikao hivyo, kwa sababu nafasi nyingi ziko wazi.

“Mfano ni ile ya Luhwavi na ya Katibu wa Halmashauri Kuu ya Taifa Idara ya Siasa na Uhusiano wa Kimataifa iliyokuwa ikishikiliwa na Dk Migiro ambaye kwa sasa ni balozi.”

Alibainisha kuwa baada ya Rais Magufuli kukabidhiwa kijiti cha uenyekiti na Rais Jakaya Kikwete, aliomba Sekretarieti iliyokuwapo kuendelea na majukumu yake, hivyo vikao hivyo huenda vikatoa majukumu kwa baadhi ya wajumbe kupewa dhamana ya uongozi.

“Pia watafanya tathmini ya utendaji kazi wa Serikali, tutarajie walioonekana kama wasaliti wakiwajibishwa, lakini kwa njia ya ‘madongo’,” alisema.

Mhadhiri mwingine wa Chuo hicho, Dk Frank Tily alisema mkutano huu utakuwa na mengi, lakini huenda moja ya ajenda kuu ikawa ni kupitia mambo yaliyofanywa na Serikali ili kubaini ilipojikwaa.

“Kwa sasa kila mwananchi analia hali ngumu ya maisha, bila shaka jambo hili litateka zaidi vikao hivyo. Suala la uchaguzi wa ubunge   Dimani lazima itakuwa ajenda kubwa,” alisema.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo