Mashali taa iliyozimika ghafla


Magendela Hamisi

Bondia Thomas Mashali
KINONDONI makaburini ndiyo makazi ya mwisho hapa duniani ya bondia Thomas Mashali, ambaye enzi za uhai wake alijipachika jina la Simba Asiyefugika.

Vurugu zake zilianzia mtaani hadi kuwa bingwa wa dunia wa masumbwi kwa mkanda wa UBO na kuiweka Tanzania katika ramani nzuri ya mchezo huo.

Mashali naamini kwa kila ambaye alikuwa akimfahamu atakuwa na mengi ya kusimulia na kufunga ukurasa wa maisha ya nyota huyo wa ngumi za kulipwa nchini ambaye Oktoba 31, mwaka huu alipoteza maisha baada ya kushambuliwa kwa mapanga na matofari Kimara jijini Dar es Salaam.

Hakika kifo cha Mashali ni pigo kwa wadau wa michezo nchini, pia mazingira ya kifo chake yataendelea kuumiza vichwa vya wadau wa michezo kwani kabla ya tukio inadaiwa alifuatwa na mmoja wa watu aliokuwa akifahamiana naye ili akamsaidie kupata haki yake.

Kwa mujibu wa mashuhuda huo ndiyo ukawa mwanzo wa safari yake ya mwisho bondia huyo ambaye Novemba 19, mwaka huu alikuwa apigane pambano la kirafiki dhidi ya Denis Ronald nchini Ujerumani lililokuwa la kirafiki kwa ajili ya kumweka sawa na pambano lake la kutetea mkanda wake wa UBO dhidi ya Chimwemwe Desemba 26, mwaka huu.

Bondia huyo baada ya kuwa mtukutu uraiani katika viunga vya Tandale, Promota wa ngumi za kulipwa nchini, Kaike Siraji akamtoa mtaani na kumwingiza katika mapambano ya kulipwa na la kwanza alilicheza Novemba 27, 2009 dhidi ya Hamadu Mwalimu katika ukumbi wa Texas Manzese Dar es Salaam na kushinda kwa KO.

Waswahili wanamsemo unaosema nyota njema huonekana asubuhi kwani baada ya kushinda pambano hilo kwa KO, Aprili 4, 2010 akapanda ulingoni kwenye ukumbi wa Magomeni Kondoa kuzichapa na Karama Nyilawila ambaye kwa wakati huo alikuwa katika kiwango kizuri na kuogopwa na mabondia lukuki ndani na nje ya nchi na kufanikiwa kutoka naye sare.

Pambano lake la tatu alicheza na Robert Mrosso katika ukumbi wa DDC Kariakoo na kushinda kwa KO, Desemba 9, 2010 siku ya sherehe za Uhuru wa Tanganyika alifanikiwa kushinda pambano lake la nne dhidi ya George Dimosso.

Harakati za kujiweka sawa katika ramani ya dunia ziliendelea ambapo Aprili 9, 2012 alimtwanga Selemani Said kwa pointi na Juni 24, 2012 alimtwanga Maisha Samson kwa KO, Oktoba 14, 2012 alimtwanga bondia Med Sebyala na kubeba ubingwa wa Afrika Mashariki na Kati katika ukumbi wa Friends Corner Manzese Dar es Salaam.

Januari 12, 2013 alitetea ubingwa huo baada ya kumtwanga Bernard Mackoliech kwa KO katika ukumbi wa Friends Corner, Manzese na baada ya hapo Mei Mosi 2013, akapanda ulingoni kuwania mkanda IBF Afrika, uzito wa kati dhidi ya Francis Cheka na kupoteza kwa KO.

Julai 7, 2013 alipanda ulingoni katika pambano lake la 10, tangu aingie katika ngumi za kulipwa na kufanikiwa kumtwanga Patrick Amote wa Kenya katika pambano lisilo la ubingwa lililochezwa Uwanja wa Ndani wa Taifa, Dar es Salaam.

Baada ya kushinda pambano hilo, Agosti 30 alipanda ulingoni kuzichapa na Mada Maugo 'Mbunge wa Rorya' na kushinda kwa pointi na kupata nafasi ya kupanda ulingoni nchini Urusi Novemba 16, kuwania mkanda wa Mabara wa UBO dhidi ya Arif Magomedov na kupoteza kwa KO.

Simba Asiyefugika alipanda tena ulingoni Machi 29, 2014 dhidi ya Japhet Kaseba kuwania mkanda wa UBO Afrika uzito wa juu na kufanikiwa kushinda kwa pointi, miezi mitano baadaye akapoteza pambano lisilo la ubingwa dhidi ya Mada Maugo, ambaye alilipa kisasi kwa pointi.

Kutokana na kupoteza pambano hilo, akaendelea kujipanga na Oktoba 5, mwaka huo huo katika Uwanja wa Mkwakwani jijini Tanga akafanikiwa kumtwanga Alibaba Ramadhani kwa TKO katika pambano lisilo la mkanda. Novemba Mosi katika ukumbi wa Friends Corner akamtwanga kwa TKO, Henry Wandera.

Machi 7, 2015 katika ukumbi wa Vijana, Dar es Salaam alimtwanga kwa TKO katika pambano lisilo la ubingwa ambalo alijiweka sawa dhidi ya Abdallah Pazi ‘Dulla Mbabe’, kwa pointi kwenye Uwanja wa Ndani wa Taifa.

Baada ya kushinda pambano hilo, bondia Selemani Said akaamua kujiuliza tena na kupanda ulingoni Juni 6, na Mashali akashinda kwa KO, Pia, Agosti 29 alipanda ulingoni kuzichapa na Ibrahim Tamba na kushinda kwa alama.

Kutokana na kufanya vema, akaona ajiulize tena dhidi ya Cheka akiwa chini ya Kocha Ramadhani Uhad 'Rama Jah' katika pambano lililochezwa Desemba 25, mkoani Morogoro na kufanikiwa kushinda kwa alama na kupata nafasi ya kuwania ubingwa wa mabara uzito wa super middle nchini Urusi Machi 5, mwaka huu dhidi ya Apti Ustarkhanov na kupigwa kwa KO raundi ya pili.

Mashali baada ya kupigwa katika pambano hilo la uzito wa kati alirejea nchini kujipanga upya na Mei 14, akapanda ulingoni ukumbi wa Uwanja wa Ndani wa Taifa dhidi ya raia wa Iran, Sajjad Mehrabi na kuwania mkanda wa Dunia wa UBO uzito wa super na kufanikiwa kushinda na kunyakua ubingwa huo.

Ushindi huo ulimpa kiburi Mashali enzi za uhai wake na kusaka pambano lingine kwa maana nia yake ili kuidhihirishia dunia kuwa yeye ni Mtanzania anayefanya vema katika ndondi na kufanikiwa kupanda ulingoni Julai 9, nchini China dhidi ya Zulpikar Maimaitiali na kupoteza kwa TKO.

Pambano lake la mwisho hadi mauti yanamkuta alipigana Septemba 12, katika ukumbi wa Chee Kwa Chee Pub, Bagamoyo mkoani Pwani na kumtwanga Shabani Kaoneka.

Siku chache Mashali alizungumza na mwandishi wa makala haya na kuweka wazi mikakati yake ya kuhamia Bagamoyo akiamini huko kutampa mafanikio zaidi.

Maneno yake ya mwisho kwa JAMBO LEO

"Ndugu yangu nimeweka kambi Bagamoyo kwa ajili ya pambano langu la Desemba 26, pia moja ya mikakati yangu ni kuhakikisha nahamia Bagamoyo nimekutana na baadhi ya wadau ambao naamini nikiwa nao maisha yangu yatafanikiwa zaidi.

Pia, mikakati yangu mingine ni kuhakikisha nafanya vema katika masumbwi na ndiyo maana nimeamua kuingia mapema kambini kwani nina muda wa miezi mitatu na lengo ni kuangalia je, nikifanya mazoezi kwa kipindi kirefu hali inakuwaje kwani mara nyingi ninapokuwa na pambano naingia kambini kwa mwezi mmoja."

Mashali alizikwa Novemba 2, mwaka huu katika makaburi ya Kinondoni.

Mungu ailaze roho ya Mashali, mahali pema peponi amen.
Share on Google Plus

About Unknown

    Blogger Comment
    Facebook Comment

0 comments:

Post a Comment

Laptop City

Tangazo